Ni rasmi sasa, Kenya imeruhusu Trump kuleta wagonjwa wa Ebola nchini
WATAALAMU wa magonjwa ya kuambukiza kutoka Amerika wamewasili nchini Kenya na tayari wanaendelea na maandalizi ya kituo maalum cha Ebola ambacho Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Amerika, Marco Rubio, amesema kitaanza kufanya kazi ndani ya siku saba zijazo.
Ikulu ya White House ilithibitisha Jumatano kuwa Amerika inaandaa kile ilichokitaja kama “kituo cha kisasa” nchini Kenya kwa ajili ya kuwatenga raia wa Amerika walioathiriwa au waliokaribiana na virusi vya Ebola.
Kituo hicho kitajengwa, kuendeshwa na kuhudumiwa kikamilifu na Wamarekani bila kushirikisha maafisa wa afya wa Kenya.
Kwa mujibu wa vyanzo, kituo hicho kinajengwa karibu na maeneo ya kijeshi ya Uingereza katika Kaunti ya Laikipia.
Rais William Ruto jana aliitisha kikao cha dharura cha Baraza la Mawaziri kujadili hali ya Ebola katika ukanda huu. Hata hivyo, haikubainika ni maamuzi gani yalifikiwa katika kikao hicho. Afisa mmoja wa afya alisema kuwa kufikia wakati Baraza la Mawaziri lilikuwa likikutana, “mchakato huo tayari ulikuwa umeanza.”
“Tayari wako nchini na wanaendelea kujenga kituo hicho,” kilisema chanzo kimoja kinachofahamu moja kwa moja kuhusu mpango huo.
Muungano wa Madaktari, Wanafamasia na Madaktari wa Meno nchini Kenya (KMPDU) umepatia serikali muda wa saa 48 kueleza hadharani masharti kamili ya makubaliano yake na Amerika au ikabiliwe na mgomo wa kitaifa wa madaktari.
Katibu Mkuu wa KMPDU, Dkt Davji Bhimji Atellah, alisema kituo hicho kinaanzishwa katika Kituo cha Anga cha Laikipia.
“Kenya ni taifa huru, si eneo la kutengwa wagonjwa wa magonjwa hatari kwa maslahi ya kisiasa,” alisema Dkt Atellah.
“Hatutakubali Kenya kutumiwa kama mahali pa kuhifadhi wagonjwa wa virusi hatari ambavyo havikutoka nchi yetu.”
Muungano huo uliitaka serikali kueleza kwa nini Kenya imechaguliwa kupokea raia wa Amerika walio na Ebola ilhali mataifa jirani na maeneo yaliyoathirika zaidi hayajapewa jukumu hilo.
“Ikiwa Amerika inaamini safari ya saa 12 ya kuwarudisha raia wake Washington ni hatari sana, kwa mantiki gani ni salama kuwaleta Kenya?” alihoji Dkt Atellah.
Muungano huo pia ulisema hautakubali mfumo wa afya wa kibaguzi nchini Kenya na ukatoa masharti matatu makuu.
Kwanza, serikali ichapishe mara moja makubaliano kamili kati yake na Amerika na kueleza kwa nini Kenya ilichaguliwa.
Pili, ieleze ni kwa nini inatanguliza ujenzi wa kituo cha wageni cha magonjwa hatari ilhali hospitali za umma nchini hazina vifaa vya msingi.
Tatu, ikiwa mradi huo utaendelea, serikali itumie nafasi hiyo kuajiri maelfu ya madaktari na wauguzi wa Kenya wasio na ajira kwa masharti ya kudumu.
KMPDU ilisema haitakubali madaktari wa Kenya kutumiwa kama wafanyakazi wa bei rahisi katika mazingira hatari bila mishahara bora, marupurupu ya kazi hatari na bima kamili ya afya.
Wakati huo huo, Wizara ya Afya kupitia Katibu katika Idara ya Afya ya Umma Mary Muthoni ilisema Kenya ina uhuru wa kushirikiana na mataifa mengine katika kupambana na Ebola iliyosababisha zaidi ya vifo 100 nchini DRC.
“Kenya itashirikiana na mataifa mengine ikiwemo Amerika kuimarisha mifumo yake mradi tu iwe ndani ya sheria za nchi,” alisema Muthoni.
Alisema si jambo jipya kwa Kenya kuwa na vituo vya kutenga wagonjwa kwani hatua kama hiyo ilichukuliwa wakati wa janga la Covid-19.
Taarifa rasmi ya serikali ya Donald Trump sasa imethibitisha kuwa kituo hicho kitajengwa Kenya kwa ajili ya kuwatenga watu wanaoshukiwa kuwa wameathiriwa na Ebola.
“Amerika inafanya kazi na serikali ya Kenya na washirika wengine kuwa na kituo cha kuwahifadhi watu wasioonyesha dalili lakini wanaoshukiwa kuathiriwa na Ebola,” alisema afisa mmoja wa serikali ya Trump.
Aliongeza kuwa Kenya na Amerika zimekuwa washirika wa muda mrefu katika sekta ya afya na ushirikiano huo ni kuendeleza juhudi za pamoja dhidi ya mlipuko wa Ebola.
Hata hivyo, wataalamu wameonya kuwa kituo cha kufuatilia wagonjwa na kituo cha kutibu wagonjwa wa Ebola vina viwango tofauti vya hatari.
Kwa mujibu wa Mary Muthoni, Kenya ina kituo kimoja pekee maalum cha kutenga wagonjwa wa homa kali ya virusi katika Hospitali ya Taifa ya Kenyatta, Nairobi.
Aidha hakuna chanjo wala tiba iliyoidhinishwa kwa aina ya Bundibugyo ya Ebola inayosababisha vifo DRC na Uganda.
Vyanzo vinasema Wamarekani hawatatumia kituo hicho cha KNH bali watajenga chao binafsi na hakuna Mkenya atakayeruhusiwa kuingia humo.
Raia wa Amerika walioambukizwa watatibiwa na wataalamu wa Amerika pekee.
“Ikiwa hawataki Wakenya wachanganyikane na raia wao, kwa nini walete wagonjwa hapa?” kilisema chanzo kimoja kilicho karibu na mpango huo.
Aliyekuwa Jaji Mkuu David Maraga ametaka Bunge kuhusishwa mara moja katika suala hilo akisema hakuna ushirikiano unaopaswa kuhatarisha usalama na uhuru wa Wakenya.
Rais wa Chama cha Wanasheria Kenya (LSK) Charles Kanjama pia alisema Kenya inapaswa kukataa ombi hilo na badala yake vituo hivyo vijengwe karibu na maeneo yaliyoathirika mashariki mwa DRC au magharibi mwa Uganda.
Gavana wa Murang’a Irungu Kang’ata naye alipinga makubaliano hayo ya siri kati ya Kenya na Amerika akisema yanaweka maisha ya Wakenya hatarini.
“Kama Mkenya, siamini nia ya serikali kuingia katika makubaliano kama haya,” alisema Kang’ata.