Wasichana 6 wakamatwa kuhusiana na moto uliosababisha maafa Utumishi Girls
AFISA mmoja anayehusika na uchunguzi wa moto uliotokea katika shule ya wasichana ya Utumishi mjini Gilgil, amesema wasichana sita wanahojiwa kuhusiana na mkasa huo.
Kwa mujibu wa afisa huyo, wanafunzi hao ni wanachama wa chama cha maskauti waliokuwa wamehudhuria shughuli fulani mapema siku hiyo na wanaaminika kuingiza mafuta ya taa shuleni.
“Tunataka kubaini mafuta hayo yaliingiaje shuleni. Sababu ya kuwahoji ni kwamba eneo la tukio lilikuwa la kutisha sana. Zaidi ya miili saba ilipatikana ikiwa sehemu moja. Inaonekana wanafunzi walikuwa wakitembea kwa makundi kutokana na hofu kabla ya kuzidiwa na moto,” alisema afisa huyo.
Kati ya wanafunzi 16 waliofariki, ni miili sita pekee iliyokuwa imetambuliwa kwa mujibu wa dawati la kufuatilia familia la Shirika la Msalaba Mwekundu Kenya.
Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu wa Shule za Sekondari na Vyuo (KUPPET), Akello Misori, alituma rambirambi kwa familia zilizopoteza watoto wao huku akielezea wasiwasi mkubwa kuhusu hatua za usalama katika shule hiyo.
Katika taarifa kwa vyombo vya habari, Misori alitaka uwajibikaji kuhusu vifo hivyo akisema tukio hilo linafanana na majanga mengine ya awali katika Shule ya Wasichana ya Moi jijini Nairobi na Hillside Academy, Nyeri, ambapo sera za usalama shuleni ziliibua mjadala mkubwa.
Alisema Bodi ya Elimu ya Kaunti, maafisa wa ubora wa elimu, bodi ya shule, usimamizi wa shule pamoja na polisi wanaosimamia usalama wa shule hiyo wanapaswa kuwajibishwa.