Polisi wakamata wanafunzi wanne wanaoshukiwa kuchoma bweni Nyeri
POLISI mjini Nyeri wamewakamata wanafunzi wanne wasichana Shule ya upili ya St Paul’s Githakwa wanaoshukiwa kuchoma bweni la shule usiku wa kumkia Jumanne.
Wanafunzi hao, watatu wa kidato cha nne na mmoja wa kidato cha tatu, wanadaiwa kuwasha moto katika sehemu ya bweni la Blessed Sister Irene Nyaatha na kusababisha uharibifu wa mali ya wanafunzi 25.
Kulingana na mkuu wa shule Margaret Wambugu, tukio hilo lilianza baada ya baadhi ya wanafunzi kuripoti kupotea kwa sare zao za shule jambo lililosababisha mabishano kati ya wanafunzi wa kidato cha nne na mmoja wa kidato cha tatu aliyeshukiwa kuhusika na wizi huo.
Walimu waliingilia kati na kuwatuliza wanafunzi hao kabla ya kuwarudisha mabwenini. Baadaye usiku huo, moto ulizuka katika bweni hilo na kusababisha taharuki kubwa.
Kwa msaada wa majirani na maafisa wa polisi, moto huo ulidhibitiwa kabla haujasambaa zaidi. Kwa bahati nzuri, wanafunzi wote waliokuwa ndani ya bweni walifanikiwa kuokolewa bila majeraha.
Uchunguzi wa awali umeonyesha kuwa moto huo huenda ulipangwa mapema kutokana na hofu ya mitihani.
Aidha, ilidaiwa kuwa wanafunzi hao walipata ushawishi kutoka kwa visa vya fujo vinavyoendelea kushuhudiwa katika shule mbalimbali nchini.
Polisi walipata viberiti pamoja na chombo kilichodhaniwa kuwa na kitu kinachoweza kuwaka moto kwa urahisi. Uchunguzi zaidi kuhusu chanzo cha moto huo unaendelea.