Bonge la sakata afisa katika serikali ya Sakaja akinaswa na mabunda ya pesa nyumbani
KUKAMATWA kwa Bw Patrick Analo Akivaga, Afisa Mkuu wa Mipango ya Miji katika Kaunti ya Nairobi na mmoja wa watu waliokuwa na ushawishi mkubwa katika serikali ya Gavana Johnson Sakaja, kumegeuka kuwa sakata kubwa baada ya maafisa wa Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) kudai walipata magunia ya pesa pamoja na mali nyingine.
Analo alikamatwa katika makazi yake mtaani Syokimau katika operesheni iliyofanywa na maafisa wa EACC usiku, hatua ambayo ilifungua ukurasa mpya wa uchunguzi unaohusisha utoaji wa vibali vya ujenzi visivyo halali na mtandao wa rushwa ndani ya Kaunti ya Nairobi.
Katika msako huo, maafisa hao walidai kupata Sh51.3 milioni na dola 113,000 (takriban Sh14 milioni), ambazo zilikuwa zimehifadhiwa katika mifuko na magunia ndani ya nyumba na sehemu ya buti ya gari lake. Jumla ya fedha zilizopatikana ni takriban Sh65.3 milioni.
Pamoja na pesa hizo, maafisa wa EACC pia walinasa hati za kumiliki ardhi, hati za kumiliki magari, simu za mkononi, vipakatalishi, iPad, mikataba ya mauzo ya ardhi na magari, pamoja na ramani na vibali vya ujenzi vya Kaunti ya Nairobi.
EACC ilieleza kuwa uchunguzi huo unahusiana na madai ya mali isiyoelezeka na mtandao wa utoaji wa vibali vya majengo yasiyotimiza viwango, ambayo yamehusishwa na vifo vya watu kadhaa baada ya majengo kuporomoka jijini Nairobi.
Mkurugenzi Mtendaji wa EACC, Abdi Mohamud, alisema uchunguzi umebaini uwezekano wa mali ambayo thamani yake ni tofauti na kipato halali cha afisa huyo.

Tumeona mali na majengo ambayo hayalingani na mapato yake rasmi kwa muda aliohudumu katika Kaunti ya Nairobi,” alisema Mohamud.
Kwa miaka kadhaa, Analo amekuwa akihusishwa na idara ya Mipango ya Miji, ambapo alishikilia wadhifa wa Afisa Mkuu wa Mipango na wakati mmoja Kaimu Karani wa Kaunti, nafasi iliyompa nguvu kubwa katika maamuzi ya miradi ya mabilioni ya shilingi.
Hata hivyo, alianza kupigwa darubini kufuatia tuhuma za rushwa, hasa kuhusu jinsi vibali vya ujenzi vilivyokuwa vikitolewa bila kufuata taratibu sahihi.
Bunge la Kaunti ya Nairobi lilimhoji mwaka 2024 baada ya kubainika kuwa takriban miradi 600 ya ujenzi ilipitia mikononi mwake kwa njia zilizoibua maswali.
Baadhi ya maafisa wa chini walidai kuwa walikuwa wakipewa mamlaka ya kuidhinisha miradi kwa niaba yake, jambo lililozua utata mkubwa kuhusu nani hasa anadhibiti mfumo wa vibali vya ujenzi.
Analo alikana kuhusika moja kwa moja, akisema hakuhusika na mfumo wa idhini na kwamba hangeweza kuwajibika kwa vibali alivyodai havikupitia mikononi mwake.
Hata hivyo, madiwani walidai kuwepo kwa mtandao wa maafisa waliokuwa wakitoza kati ya Sh2 milioni na Sh10 milioni kwa kila kibali cha ujenzi, huku baadhi ya wajenzi wakiruhusiwa hata kuongeza ghorofa kinyume cha idhini ya awali.
Chama cha Wasanifu Majengo Kenya pia kilishutumu kaunti kwa kuvuruga mfumo wa kidijitali wa vibali, jambo lililoruhusu maafisa kuidhinisha maombi kwa mikono na hivyo kufungua mianya ya rushwa.
Zaidi ya hayo, ilidaiwa kuwa baadhi ya majengo yaliidhinishwa hata baada ya kukataliwa na kamati za kiufundi za mipango ya mji, hali iliyoongeza hofu kuhusu usalama wa majengo jijini.
Ripoti ya Ofisi ya Malalamishi ilipendekeza hatua za kisheria dhidi ya baadhi ya maafisa wa Nairobi, akiwemo Analo, kwa madai ya kutoa vibali kabla ya taratibu kukamilika na kushindwa kutekeleza maagizo ya kusitisha ujenzi haramu.
Kukamatwa kwake kunajiri baada ya Nairobi kukumbwa na mfululizo wa majengo kuporomoka, ambapo zaidi ya watu 11 tayari wamepoteza maisha katika matukio tofauti.
Baada ya kuporomoka kwa jengo la ghorofa 16 kwenye barabara ya Muhoho, uchunguzi ulibaini kuwa jengo hilo lilikuwa limeidhinishwa kujengwa orofa 12 pekee lakini ujenzi uliendelea kinyume cha sheria.