Uchunguzi wa bunge kuhusu mahali zilikoelekezwa Sh6.3bn za eCitizen wakwama
UCHUNGUZI wa Bunge la Kitaifa kuhusu kuelekezwa kwa Sh6.3 bilioni, mapato ya mtandao wa eCitizen hadi Benki ya Equity, umekwama.
Hii ni baada ya Mkaguzi wa Hesabu za Serikali kuanika jinsi fedha zilivyohamishwa bila utaratibu kufuatwa, jambo ambalo lilifanya wabunge kuzua maswali kuhusu uwajibikaji.
Hata hivyo, Kamati ya Ukaguzi wa Pesa za Umma katika Bunge la Kitaifa ambayo ilikuwa ikichunguza ukora huo, imekimya baada ya wanachama kughairi nia kuhusu kusikizwa kwa kesi hiyo.
Kwa mujibu wa notisi ya kamati, Mwenyekiti wa PAC Tindi Mwale ambaye ni Mbunge wa Butere, alikuwa amepanga mkutano mnamo Mei 5, 2026.
Kikao hicho ambacho hakikufanyika kilikuwa cha kukutana na kampuni zinazohusishwa na mtandao wa eCitizen zikiwemo Electronic Citizen Solutions, Pesaflow, Webmasters, Olive Tree Media na Goldrock.
Mkutano ambapo wanachama wangekutana na meneja mkurugenzi wa Benki ya Equity nao uliahirishwa. Hii ni baada ya waliofaa kufika, kuomba muda zaidi wa kujiandaa kabla ya kuwasilisha stakabadhi zilizohitajika.
Kamati hiyo iliratibisha mkutano hadi Mei 12, 2026 lakini haikutoa ufafanuzi kwa nini haukufanyika tena.
Zaidi ya mwezi mmoja baadaye kamati hiyo haijakutana na kuzua maswali mengi kuhusu mustakabali wa uchunguzi huo.
Baadhi ya wanachama ambao hawakutaka kutajwa walizua maswali kuhusu maelezo yaliyosababisha mkutano wa Mei kuahirishwa.
Hii ni kwa sababu kampuni kadhaa tayari zilikuwa zimewasilisha stakabadhi zao kwa kamati.
Mwanachama mmoja aliuliza kwa nini muda zaidi ulihitajika huku mwengine akisema waliostahili kuwasilisha waliarifiwa kuhusu maswali tata ambayo wabunge wangeuliza.
Ukaguzi wa hesabu wa mwaka wa kifedha 2021/22 hadi 2023/24, ulibaini kuwa akaunti kwa jina Pesaflow katika Benki ya Equity ilipokea Sh6.24 bilioni.
Katika mwaka wa kifedha wa 2020/21 Sh7.84 milioni ziliwekwa kwenye akaunti hiyo pamoja na dola za Kimarekani 5.86 milioni.
Katika mwaka wa kifedha wa 2021/22 pesa ambazo ziliwekwa zilikuwa Sh60.88 milioni pamoja na dola 29.73 milioni.
Mwaka uliofuatia wa kifedha wa 2022/2, dola 12.6 milioni ziliwekwa kwenye kaunti hiyo ya Equity ingawa hakuna pesa ambazo ziliwekwa mwaka uliofuatia wa 2023/24.
Afisi ya mkaguzi ilisema Equity ilikosa kutoa stakabadhi za benki kuonyesha nani alinufaikia hela hizo na iwapo zilitolewa baada ya kuwekwa.
Pia afisi ya mkaguzi ilisema nambari ya Paybill ya 222222 ambayo inatumiwa kutuma malipo baada ya kuhudumiwa kwenye eCitizen, ni rahisi kuvurugwa.
Aidha iligunduliwa kuwa pesa ambazo zinaweza kufikia Sh127.9 milioni zilitumwa kwa baadhi ya kampuni za kibinafsi bila stakabadhi kinyume na katiba.