Kilichofanya Katibu Julius Bitok kuondolewa Wizara ya Elimu
DURU kutoka Jogoo House sasa zinaashiria kwamba uhasama umekuwa ukitokota kati ya Waziri wa Elimu Julius Ogamba na aliyekuwa Katibu wa wizara hiyo Julius Bitok kabla ya kuhamishwa katika Idara ya Utalii.
Maswali yalizuka kuhusu namna Prof Bitok alivyokabili changamoto zilizoibuka katika sekta ya elimu.
Aidha, alilaumiwa kwa kutilia maanani zaidi kupigia debe azma yake ya kugombea ugavana katika Kaunti ya Uasin Gishu, kiti alichopoteza kwenye uchaguzi wa chama cha UDA 2022.
Jumanne adhuhuri, Prof Bitok aliandamana na bosi wake, Waziri Ogamba kwenye mkutano na Naibu Rais Kithure Kindiki katika afisi yake kwenye jumba la Harambee House Annex, Harambee Avenue.
Alihudhuria kikao hicho katika hadhi yake kama Katibu wa Wizara ya Elimu anayesimamia Elimu ya Msingi.
Mkutano huo ulikusudiwa kutafuta suluhisho kuhusu fujo zilizoenea kote nchini ambazo zimeathiri shule 204, kwa mujibu wa takwimu rasmi.
Prof Kindiki alitoa mawasiliano akiamuru Wizara ya Elimu kulainisha usalama shuleni na utekelezaji wa sheria ili kudhibiti shughuli za elimu kutatizwa.
Wizara vilevile iliagizwa “kuunda mikakati ya kushirikisha wadau, kubuni mapendekezo ya kulainisha utoaji huduma shuleni na usalama wa jamii ya shule.”
Hata hivyo, takriban saa moja unusu baada ya kurejea Jogoo House, mawasiliano kutoka kwa Mkuu wa Wafanyakazi wa Umma, Felix Koskei, yalitangaza kuwa Rais William Ruto “amemhamisha” Profesa Bitok katika Idara ya Utalii.
Atabadilishana afisi na John Lekakeny Ololtuaa ambaye sasa atasimamia Idara ya Elimu ya Msingi.
Je, Rais alihisi Profesa Bitok siye mtu anayefaa kusimamia utekelezaji wa maagizo yaliyotolewa?
Haya ndiyo mabadiliko pekee katika kiwango hicho tofauti na hatua nyinginezo za uhamisho zinazoathiri mawaziri na makatibu wa wizara wengi.
Usiku, afisi ya Bw Ogamba ilitoa taarifa kuhusu kikao na vyombo vya habari “kuzungumzia masuala yanayoathiri sekta ya elimu.”
Tukio moja lililotajwa ni wakati Profesa Bitok alitangaza kuwa Wizara ya Elimu imeagiza walimu wakuu wa shule za sekondari kujadiliana na wanafunzi ikiwa hawataki kufanya mitihani.