KRA kuanza kuwinda waajiri wanaoshikilia Sh100 bilioni ushuru wa Nyumba Nafuu
MAMLAKA ya Ukusanyaji Ushuru Kenya (KRA) inatarajiwa kuanza msako dhidi ya waajiri waliokata ushuru wa Mpango wa Nyumba Nafuu kutoka kwa wafanyakazi wao lakini wakashindwa kuuwasilisha serikalini, huku kiwango kinachodaiwa kufikia zaidi ya Sh100 bilioni.
Hatua hiyo inajiri baada ya Idara ya Serikali ya Nyumba kuomba Bunge kurekebisha Mswada wa Fedha wa mwaka 2026 ili kumpa Kamishna Mkuu wa KRA mamlaka ya kisheria ya kufuatilia na kukusanya fedha ambazo hazijawasilishwa.
Akizungumza mbele ya Kamati ya Bunge ya Fedha na Mipango ya Kitaifa wakati wa ukusanyaji wa maoni kuhusu Mswada wa Fedha 2026, Mwenyekiti wa Bodi ya Hazina ya Nyumba Nafuu Jeremiah Simu alisema zaidi ya Sh100 bilioni zimefichwa na waajiri tangu ushuru huo ulipoanzishwa.
Wakati huo huo, mamia ya familia katika maeneo ya mashambani Kaunti ya Trans Nzoia wanaishi bila vyoo, hali inayowalazimu kutumia maeneo ya wazi kujisaidia na hivyo kuhatarisha afya ya jamii.
Maafisa wa afya wa kaunti hiyo wametaja Wadi ya Keiyo kama eneo lililoathirika zaidi, huku vijiji 12 vikiwekwa kwenye orodha ya maeneo yenye hatari kubwa kutokana na kiwango cha chini cha umiliki wa vyoo na tabia ya kujisaidia ovyo.
Kutokana na hali hiyo, Idara ya Afya ya Umma imeanzisha kampeni kabambe za kuhamasisha wananchi kuhusu umuhimu wa usafi na kuwahimiza kujenga vyoo vya kisasa majumbani.
Maafisa wa afya wanaonya kuwa ukosefu wa huduma bora za usafi unaendelea kuwaweka wakazi katika hatari ya kuambukizwa magonjwa mbalimbali yanayosababishwa na maji machafu.