Habari za Kitaifa

Polisi wachunguza mtandao wa kusajili vijana kujiunga na ISIS

Na BRIAN OCHARO June 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

POLISI wanachunguza tetesi kuhusu usajili wa vijana kujiunga na makundi ya ugaidi kimataifa Pwani, baada ya washukiwa wawili kukamatwa.

Wawili hao wamefunguliwa mashtaka ya kuhusika na usajili wa wapiganaji wa kundi la kigaidi la ISIS nchini Msumbiji.

Yusuf Mbashir Swaleh na Abdulkarim Mohamed Salim walifikishwa mbele ya Mahakama ya Kwale ambapo walikana mashtaka kadhaa yanayohusiana na ugaidi.

Mashtaka hayo ni pamoja na kuratibu na kuwezesha uajiri wa wanachama wa kundi hilo la kigaidi pamoja na kuandaa mikutano ya uajiri inayolenga kupanua mtandao wake wa uungwaji mkono nchini.

Bw Swaleh anakabiliwa na mashtaka kadhaa chini ya Sheria ya Kuzuia Ugaidi, yakiwemo kufadhili safari za kigaidi, kumiliki vifaa vinavyohusiana na ugaidi pamoja na kukusanya taarifa za itikadi kali.

Mahakama iliambiwa kuwa, mnamo Mei 7, 2026, mshukiwa huyo anadaiwa kutuma Sh8,000 kupitia simu kwa Abdulkarim Salim ili kuwezesha safari ya kwenda Msumbiji kwa lengo la kujiunga na kundi la Islamic State (ISIS).

Anadaiwa pia kupatikana na simu aina ya Samsung Galaxy A15 iliyokuwa na taarifa za kueneza itikadi kali, ikiwemo video na sauti zinazodaiwa kuhamasisha matumizi ya vita na itikadi za kigaidi.

Kwa upande wake, Bw Salim anakabiliwa na mashtaka ya kuandaa mikutano ya uajiri, kuwezesha uajiri wa wanachama wa kundi la kigaidi pamoja na kumiliki mali iliyotumika katika kutekeleza vitendo vya kigaidi.

Mahakama ilielezwa kuwa, kabla au mnamo Mei 18, 2026, alidaiwa kuandaa mkutano katika eneo la Jua Kali, Mombasa, uliolenga kuchangisha fedha kwa ajili ya kusaidia kundi la kigaidi.

Anadaiwa pia kusaidia uajiri katika mtandao wa Islamic State pamoja na kutumia simu ya mkononi kuratibu shughuli zinazohusiana na itikadi kali.

Upande wa mashtaka ulipinga ombi la dhamana, ukieleza kuwa washtakiwa hao wanaweza kutoroka wakiachiliwa kwa dhamana.

Mahakama pia iliambiwa kuwa, watu hao wana uwezo wa kutoroka kwani wana uhusiano na watu walioko Msumbiji pamoja na historia ya kukamatwa nchini Tanzania.

Mahakama iliambiwa wachunguzi wanaamini washtakiwa wanaweza kutumia njia zisizo rasmi za mipakani kutoroka, huku uhusiano wao na watu walioko Msumbiji ukiongeza uwezekano wa kutoweka.

Serikali ilieleza pia kuwa washtakiwa hawana makazi yanayojulikana wala ajira rasmi, jambo linalowafanya kuwa vigumu kupatikana endapo wataachiliwa huru.

Mahakama pia ilielezwa kuwa washtakiwa wana pasipoti za Kenya na uwezo wa kutumia majukwaa ya kidijitali, hali inayoweza kuwezesha kutoroka au kuingilia uchunguzi unaoendelea.

Upande wa mashtaka ulionya kuwa, ushahidi mwingi ni wa kidijitali na unaweza kuingiliwa iwapo washtakiwa watapewa dhamana.

Ilielezwa pia kuna vijana kadhaa ambao tayari wameingizwa kwenye mtego huo na wako katika hatua mbalimbali za maandalizi ya kusafiri kwenda Msumbiji.

Upande wa mashtaka ulisema hali hii inazua wasiwasi wa kiusalama iwapo washtakiwa wataachiliwa.

Mpelelezi wa Kitengo cha Kupambana na Ugaidi (ATPU) Pharis Kinyua alieleza kuwa kuna ushahidi wa kutosha unaowaunganisha washtakiwa na mtandao mpana wa uajiri na uratibu wa shughuli za kigaidi.

Afisa huyo alisema washtakiwa walikamatwa katika mpaka wa Horohoro na maafisa wa Tanzania wakiwa njiani kuelekea Msumbiji kujiunga na wapiganaji wa ISIS.

Upelelezi unaoendelea, aliiambia mahakama, umebaini makosa kadhaa ya kigaidi na akasisitiza kuwa kuwaachilia huru kunaweza kuathiri mashahidi na uchunguzi.

Mahakama pia ilielezwa kuwa wachunguzi wanahofia huenda shughuli hizo zikaenea miongoni mwa vijana walio katika hatua mbalimbali za kuandaliwa kujiunga na mtandao huo.

Kinyua aliongeza kuwa vyombo vya usalama bado vinafuatilia watu wengine wanaodaiwa kusajiliwa lakini ambao bado hawajasafiri kwenda Msumbiji.

“Kwa kuzingatia usalama wa washtakiwa, tunaomba wanyimwe dhamana kwa sababu wakiachiliwa watawindwa na wanachama wa kundi lao la kigaidi ili kuwanyamazisha wasifichue taarifa kuhusu operesheni za kigaidi,” alisema.

Kesi hiyo itatajwa tena Juni 18, wakati mahakama ikitarajiwa kutoa uamuzi kuhusu ombi la dhamana huku uchunguzi ukiendelea kuhusu mtandao unaodaiwa kuhusisha Kenya na seli za ISIS nchini Msumbiji.