Mkuu wa kuwalinda mashahidi aagizwa afike mahakamani leo
MAHAKAMA Kuu jana ilimwaamuru Mkurugenzi wa Mamlaka ya Kuwalinda Mashahidi (WPA) kufika kortini leo, kueleza hatua zilizochukuliwa kuwalinda mashahidi katika kesi ya kutoweka kwa wanaharakati wanne wa Mathare.
Jaji Alexander Muteti alimwamuru mkurugenzi huyo kufika binafsi kortini Agosti 18, 2026, ili kutoa maelezo kuhusu ulinzi wa mashahidi wanaohusishwa na kesi hiyo.
Wanaharakati hao, Abdul Aziz Zizu, MacMillan Kiarie, Michael Oloo na Evans Oloo, walitekwa nyara Juni 20 na wanaume waliokuwa wamevalia barakoa na kuficha nyuso zao.
Mawakili Abner Mango, Noordeen Khagai na Pius Oyoo waliambia mahakama kuwa walifika katika afisi za WPA lakini hawakupewa taarifa kuhusu mashahidi waliowasilisha majina yao.
“Tulienda kwa afisi za WPA lakini hatukupata msaada wowote. Hatukuelezwa ikiwa mashahidi hao wamehojiwa na kuwekwa mahali salama ili wasitishwe na maafisa wa usalama,” alisema Mango.
Jaji Muteti aliamuru WPA kuwalinda mashahidi na kuhakikisha wanatoa ushahidi bila kuhofia usalama wao.
Mahakama pia iliagiza maafisa Brenda Akoth Opondo, Waceke Macharia na Jane Nyambura Njoroge kufika kutoa ushahidi kuhusu kutoweka kwa wanaharakati hao.
Afisa wa polisi Humphrey Kaimenyi aliagizwa kuwasilisha kanda za CCTV zinazoonyesha matukio yaliyopelekea kutoweka kwao.
Awali, Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja na Mkurugenzi wa DCI Mohamed Amin waliambia mahakama kuwa wanaharakati hao “hawako mikononi mwa polisi.”
Jaji Muteti alisema mahakama ina jukumu la kuhakikisha ukweli unapatikana na haki inatendeka kwa mujibu wa Katiba.