Dondoo

Wanakijiji wapumua baada ya mchawi kuamua kuokoka

Na MWANDISHI WETU June 24th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

SINOKO, Bungoma:

WAKAZI wa kijiji kimoja walipumua baada ya jamaa aliyekuwa na tabia za urogi na kukimbia usiku, alipoamua kuacha vituko hivyo na kuokoka.

Mchawi huyo alikuwa gumzo kutokana na desturi yake ya kuzurura usiku wa manane akibisha milango ya watu na kuwatia hofu.

Wakazi wengi walimhusisha na vitendo vya ushirikina.

Lakini mambo yalibadilika alipojitokeza hadharani katika mkutano wa krusedi na kushuhudia jinsi maisha yake yalikuwa yamejaa mateso na upweke ajabu.

Alikiri kwamba alichoshwa na visanga vyake vya kukimbia gizani na kuishi kwa hofu ya kutengwa na jamii.

Tangu aokoke polo amekuwa akihudhuria ibada mara kwa mara na kuhimiza vijana waepuke mienendo inayowatenganisha na jamii.

Wakazi sasa wanasema kijiji chao kimepata utulivu na kwamba kelele za usiku zilizowahangaisha kwa muda mrefu zimebaki historia.