Habari za Kitaifa

Mishahara kwanza, maendeleo baadaye yageuka kauli mbiu ya serikali za kaunti

Na COLLINS OMULO June 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KAUNTI tisa nchini zimetumia chini ya asilimia 20 ya bajeti zao za maendeleo katika miezi tisa ya kwanza ya mwaka wa kifedha wa 2025/2026, huku nyingi zikielekeza sehemu kubwa ya fedha kwa mishahara, marupurupu na matumizi mengine.

Ripoti mpya ya Mdhibiti wa Bajeti, Dkt Margaret Nyakang’o, inaonyesha kuwa kaunti za Kajiado, Lamu, Siaya, Uasin Gishu, Baringo, Tana River, Nakuru, Migori na Mombasa ndizo zilizorekodi matumizi ya chini zaidi ya fedha za maendeleo.

Kajiado iliongoza kwa kutumia asilimia tisa pekee ya bajeti yake ya maendeleo, ikifuatiwa na Lamu kwa asilimia 11.

Siaya na Uasin Gishu zilitumia asilimia 13, huku Baringo na Tana River zikirekodi asilimia 17.

Nakuru ilitumia asilimia 19, wakati Migori na Mombasa zikitumia asilimia 20.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, kaunti 43 zilitumia zaidi ya nusu ya fedha zao kwa mishahara, marupurupu na gharama za kila siku, jambo linaloendelea kudhoofisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayolenga kuboresha maisha ya wananchi.

Baringo ni miongoni mwa kaunti zilizotajwa katika ripoti hiyo kwa matumizi ambayo yameibua maswali kuhusu vipaumbele vya matumizi ya fedha za umma.

Katika mwaka uliopita, wakandarasi walitelekeza ujenzi wa madarasa 11 ya elimu ya chekechea wakidai serikali ya kaunti haijalipa deni la Sh6 milioni.

Madarasa hayo yako katika maeneo ya Kaplop, Kaburwo, Chesakam, Chemayes, Noswo, Borokwo, Sau, Mwal, Ketukoi na Toplen.

Katika kipindi hicho hicho, serikali ya kaunti ilitumia Sh9 milioni kwa muda wa mawasiliano ya simu kwa maafisa wake.

Aidha, ilitumia Sh510,000 kujenga choo kimoja katika eneo la Maji Mazuri na Sh500,000 kujenga vibanda viwili vya waendesha bodaboda katika maeneo ya Hilltee na Maji Mazuri.

Ripoti inaonyesha kuwa kufikia Machi 31, 2026, kaunti zote nchini zilikuwa zimetumia Sh72 bilioni pekee kati ya Sh234.3 bilioni zilizotengwa kwa maendeleo.

Hii inawakilisha kiwango cha utekelezaji wa asilimia 31 pekee.

Ni kaunti nne pekee ambazo ni Nandi, Meru, Wajir na Marsabit zilizotumia zaidi ya nusu ya bajeti zao za maendeleo katika kipindi hicho.

Wakati huo huo, kaunti 22 ziliripoti miradi 237 iliyokwama yenye thamani ya jumla ya Sh13.66 bilioni.

Kati ya fedha hizo, Sh5.11 bilioni tayari zilikuwa zimelipwa kabla ya miradi hiyo kukwama.

Dkt Nyakang’o amesema serikali za kaunti zinapaswa kupatia kipaumbele miradi iliyokwama kwa kutenga fedha za kutosha ili ikamilishwe na kuanza kuhudumia wananchi.

Pia alizitaka kutatua migogoro kuhusu mikataba na kulipa madeni halali kwa mujibu wa sheria.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, kaunti bado zinakabiliwa na madeni ya Sh156.84 bilioni, ambapo Sh116.50 bilioni ni ya matumizi ya kawaida na Sh40.34 bilioni ni ya miradi ya maendeleo.

Mdhibiti wa Bajeti alionya kuwa licha ya maendeleo yaliyopatikana katika baadhi ya maeneo, changamoto za usimamizi wa fedha, ucheleweshaji wa miradi na uratibu hafifu wa taasisi zinaendelea kuathiri utoaji wa huduma kwa wananchi na kutatiza utekelezaji wa bajeti za kaunti.