DCI sasa kuweka rekodi za wanafunzi wanaochoma shule
KATIBU wa Elimu ya Msingi, Bw John Ololtuaa, ametoa onyo kali kwa wanafunzi wa shule za upili wanaohusika na visa vya uchomaji wa shule, akisema tabia hiyo imechangia vifo vya wanafunzi 18 na kuharibu taasisi nyingi za masomo nchini.
Aidha, aliwaonya wanafunzi kuwa serikali inafuatilia mienendo yao na kwamba rekodi za utovu wa nidhamu zinaweza kuhifadhiwa na Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI).
Bw Ololtuaa alitaja matukio hayo kuwa ya kusikitisha na yasiyokubalika, akiwataka wanafunzi kuachana na vitendo vya uharibifu na badala yake kukuza uzalendo.
“Yale yanayotokea lazima yakome. Ni nchi gani nyingine duniani ambapo wanafunzi huchoma shule zao? Tunapaswa kujipenda na kuipenda nchi yetu. Tuachane na visa vya uchomaji shule,” alisema.
Aidha, aliwataka wadau wa elimu kuacha kulaumiana na badala yake kutafuta suluhu za kudumu kwa tatizo la utovu wa nidhamu unaoshuhudiwa katika shule nyingi.
Bw Ololtuaa aliwasifu wakuu wa shule kwa juhudi wanazoweka katika kusimamia nidhamu na kuhakikisha usalama wa wanafunzi licha ya changamoto zinazowakabili.
Alihoji wanafunzi iwapo wanaweza kuchoma nyumba za wazazi wao kila wanapokumbana na matatizo nyumbani, akisisitiza kuwa mali ya shule inapaswa kuheshimiwa.
Katibu huyo alisema nidhamu ya wanafunzi ni jukumu la pamoja linalohusisha wazazi, walimu na jamii kwa ujumla.
Alisisitiza kuwa wazazi wanapaswa kushiriki kikamilifu katika malezi ya watoto wao badala ya kuachia shule jukumu hilo pekee.
Akikumbuka alipokuwa mkuu wa shule, Bw Ololtuaa alisimulia jinsi alivyowahi kuzima maandamano ya wanafunzi waliokuwa wakielekea kituo cha polisi kumuokoa mwanafunzi mwenzao waliodhani alikuwa akiteswa.
“Nilipowauliza walipata habari hizo wapi, walisema tu waliambiwa. Niliwachukua wanafunzi watatu kwenda kituoni kuthibitisha madai hayo huku wengine wakirejea shuleni. Tulipofika tulimkuta mwanafunzi huyo akinywa chai na maandazi pamoja na maafisa wa polisi. Wenzake waliposikia ukweli waliomba msamaha na kuahidi kutorudia kosa hilo,” alisema.
Kulingana na Bw Ololtuaa, kisa hicho kinaonyesha umuhimu wa mazungumzo na uongozi wa busara katika kutatua migogoro ya wanafunzi.
Takwimu za Wizara ya Elimu zinaonyesha kuwa tangu Aprili 27 mwaka huu, kumekuwa na visa 330 vya fujo shuleni, vikiwemo visa 95 vya moto na majaribio 34 ya kuchoma shule.
Matukio hayo yamesababisha vifo vya wanafunzi 18 na kuibua wasiwasi kuhusu usalama katika taasisi za masomo.
Ili kukabiliana na changamoto hiyo, wizara imeahidi kuimarisha huduma za ushauri nasaha na afya ya akili shuleni.
Bw Ololtuaa pia alizitaka taasisi za kidini kushirikiana na wizara katika kuwaelimisha wazazi kuhusu wajibu wao wa kuwalea watoto kwa misingi ya maadili na nidhamu.