Msining’inie koti langu, Oburu aambia wawaniaji wa ODM 2027
KIONGOZI wa ODM, Dkt Oburu Oginga, amewaonya wawaniaji wanaodhani watapata tikiti ya moja kwa moja akisema lazima wajitetee kwa raia kupitia utendakazi wao.
Dkt Oginga amesema kuwa hatamuidhinisha kiongozi yeyote na mara hii uteuzi wa ODM utakuwa huru na haki.
Amewaonya wanaolenga kununua tikiti ya ODM kwa kupiga kambi katika makao makuu ya chama kuwa jukumu la kuwachagua raia lipo mikononi mwa wananchi na si ODM.
“Msipoteze wakati wenyu mkipiga kambi katika makao makuu ya chama ukisaka tikiti. Nenda ujitetee kwa raia kwa sababu wao ndio wataamua viongozi,” akasema Dkt Oginga.
Kiongozi huyo alikiri kuwa wakati wa marehemu ndugu yake Raila Odinga baadhi ya viongozi walikuwa wakitegemea kuidhinishwa au kusaidiwa lakini yeye hana uwezo huo.
Dkt Oginga mwenyewe amesema kuwa yupo tayari kupambania tikiti ya kutetea kiti chake cha Useneta wa Siaya, ambacho kinamezewa mate pia na aliyekuwa Gavana wa Siaya Amoth Rasanga.
“Msinitegemee kwa sababu sitawasaidia. Sitakubali mtu yeyote aning’inie koti langu kwa sababu wanaotoa tikiti kwa viongozi ni wananchi,” akasema.
Katika chaguzi za nyuma, kuwahi tikiti ya ODM hasa Nyanza, Pwani na Magharibi kumekuwa kukichukuliwa kama kunusia wadhifa unaowania hata kabla ya kura kupigwa.
Hii ni kwa sababu waliokuwa wakiwahi tikiti walikuwa wakichaguliwa kwa kura nyingi katika uchaguzi mkuu.
Marehemu Bw Odinga alikuwa na mazoea ya kuwapatanisha wagombeaji ili mmoja wao apewe tikiti ya moja kwa moja.
Mara nyingine, Raila alikuwa akifika mkutanoni na kuinua mkono wa kiongozi mmoja na kuwataka raia kuwachagua.
Hata hivyo, baada ya uchaguzi baadhi ya viongozi wa ODM wamekashifiwa kwa uzembe na utendakazi duni wakifahamu uchaguzi unaofuata tena wataungwa mkono.
Makao makuu ya ODM nayo yameshutumiwa vikali katika chaguzi za nyuma kwa kuandaa uteuzi usiokuwa na uwazi huku pia baadhi ya viongozi wakinunua tikiti ya chama.