Habari

Wetangúla akemewa kwa kumwidhinisha Nakhumicha kuwania ugavana Trans Nzoia

Na CECIL ODONGO June 29th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HATUA ya Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetangúla, kumuidhinisha Waziri wa zamani, Susan Nakhumicha, kuwania ugavana Trans Nzoia kumechemsha viongozi wa vyama tanzu ndani ya Kenya Kwanza katika kaunti hiyo na Bungoma.

Viongozi wa UDA kutoka kaunti hizo mbili wamepinga kauli ya Bw Wetangúla kuwa Kenya Kwanza itakuwa tu na mgombeaji wa Ford Kenya pekee katika ugavana wa Trans Nzoia.

Spika alimuidhinisha Bi Nakhumicha mnamo Juni 21 katika mkutano ambao pia ulihudhuriwa na viongozi wa kijamii akisema ndiye anatosha kumngóa Gavana George Natembeya.

“Ndiye mwaniaji wa Kenya Kwanza na Serikali Jumuishi kwa Ugavana hapa Trans Nzoia,” akasema Bw Wetangúla.

Mbunge wa Kiminini, Kakai Bisau, anayewania ugavana kupitia UDA na aliyekuwa Mbunge wa eneo hilo, Chris Wamalwa, wamepinga wazo kuwa Bi Nakhumicha ndiye mgombeaji wa Kenya Kwanza.

Kwenye mahojiano na Taifa Leo, Bw Bisau alisema Bi Nakhumicha hana umaarufu wowote na kukataa pendekezo la Ford Kenya aliodai ni kumlazimishia raia.

“Wetangúla kuchanganyikiwa kutagharimu Kenya Kwanza kiti hiki. Apambane aunde mambo yake Bungoma kabla kuja hapa na kutuamulia nani atakuwa gavana,” akasema Bw Bisau ambaye aliwania ugavana mnamo 2017.

“Mnamo 2022, Nakhumicha alipata kura 32,000 alipotaka kuwa mbunge mwakilishi wa kike na akashindwa. Hizo ni idadi sawa na kura nilizoshinda nayo ubunge Kiminini,” akaongeza.

Mbunge huyo alishinda kiti cha ubunge wa Kiminini kupitia DAP-Kenya mnamo 2022 lakini amekosana na uongozi wa chama hicho cha Eugene Wamalwa na sasa analenga ugavana kupitia UDA.

Ingawa hivyo, Bw Wetangúla amemtaka Bw Bisau ajiunge na Ford Kenya na apambane na Bi Nakhumicha kwenye uteuzi kama anataka aungwe mkono na Kenya Kwanza.

“Ukija Ford Kenya, utapambana na Nakhumicha kwenye uteuzi lakini usipojiunga na chama chetu, basi Nakhumicha ndiye mwaniaji wetu,” akasema Bw Wetangúla.

“Haongei kwa niaba ya UDA na nimemuuliza Pukose (Mbunge wa Endebes) kuhusu madai ya spika kuwa Kenya Kwanza itamuunga mkono mgombeaji wa Ford Kenya na akasema hana habari kuhusu makubaliano kama hayo,” akasema Bw Bisau.

Katika kaunti jirani ya Bungoma, Ford Kenya inaonekana haina mgombeaji maarufu wa ugavana huku Mbunge wa Kimilili, Didmus Barasa, wa UDA na mwenzake wa Westlands, Tim Wanyonyi, wakionekana kifua mbele.

Bw Wanyonyi amewahi kunukuliwa akisema hawezi kuwania kupitia Ford Kenya.

“Badala ya kuonyesha udikteta anastahili awe anawaunganisha viongozi. Nakhumicha hata akiungwa mkono hawezi kumshinda Natembeya,” akasema Bw Bissau.

Bw Chris Wamalwa naye ameshutumu Bw Wetangúla na kusema yuko tayari kufika debeni akisema ana imani atawahi ugavana.

Baadhi ya wabunge kutoka Kaunti ya Bungoma nao wamewataka Mabw Bisau na Wamalwa wamuunge mkono Bi Nakhumicha.