Habari

Sheria za ukaguzi wa magari yazua hasira miongoni mwa Wakenya

Na ERIC MATARA na LABAAN SHABAAN June 29th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MPANGO wa serikali kulazimisha magari ya kibinafsi kufanyiwa ukaguzi kila mwaka umezua hisia kali miongoni mwa umma, huku waendeshaji magari na viongozi wa upinzani wakitaka ukomeshwe na kuishutumu serikali kwa kuwatwika mzigo mwingine Wakenya wanaopambana na hali ngumu.
Masharti mapya yanapanua pakubwa mfumo wa wa ukaguzi wa magari nchini kwa kuamuru magari yote ya kibinafsi yanayozidi miaka minne toka tarehe ya kuundwa kufanyiwa vipimo kila mwaka kuhusu ufaafu wake barabarani.
Waendeshaji wa magari watakaokosa kupeleka magari yao kukaguliwa watakabiliwa na tishio la kushtakiwa, kutozwa faini ya hadi Sh20,000, kifungo gerezani kwa hadi miezi sita na katika baadhi ya visa, kupoteza haki ya kutumia magari kwenye barabara nchini. Sheria hizo zilizopangiwa kuanza kutekelezwa Julai 1, 2026, zilitangazwa Ijumaa iliyopita kupitia notisi ya NTSA.
“Wakenya wote wanaomiliki magari ya miaka zaidi ya minne kutoka tarehe ya kuundwa wanatarajiwa kujiandaa kwa ukaguzi kupitia tovuti ya NTSA katika eCitizen,” alisema Mkurugenzi wa NTSA, Nashon Kondiwa katika notisi. Ukaguzi huo utamgharimu mwenye gari hadi Sh2,000 kila mwaka.
Hatua hiyo imefuatia utekelezaji wa Sheria kuhusu Trafiki (Ukaguzi wa Magari), 2026, zilizochapishwa katika Notisi Rasmi Nambari 13 ya 2026 Fabreuari.
Hata hivyo, amri hiyo imekumbwa na pingamizi kali.
Muungano wa Waendeshaji Magari (MAK), kupitia msemaji wake Peter Murima, ulikataa sheria hizo mpya na kuitisha zisitishwe hadi mchakato wa kina wa kukusanya maoni ya umma utakapofanyika.
“Tunataka ushirikishaji mwafaka wa umma kabla sheria zozote kama hizo kutekelezwa. Ada hizo si za haki na ni mzigo wa ziada kwa waendeshaji magari,” alisema Bw Murima.
Viongozi wa upinzani na wadau wanahoji kuwa mpango huo unatekelezwa pasipo kushirikisha umma kikamilifu wakitaka usitishwe.
Naibu Kinara wa chama cha Jubilee Fred Matiang’i jana alikosoa sheria mpya za ukaguzi akisema zitawalimbikizia magumu zaidi Wakenya ambao tayari wanataabika.
Kinara wa Democracy for Citizens Party (DCP), Rigathi Gachagua vilevle alipinga sheria hizo akizitaja za kibaguzi na zisizohitajika.
Akizungumza kutoka makazini mwake Wamunyoro, Kaunti ya Nyeri alipowakaribisha wagombea kutoka Laikipia, Bw Gachagua alitishia kuwakusanya Wakenya kupinga sheria hizo mpya iwapo hazitaachwa kutekelezwa.