Habari

Mwanawe Museveni afunga runinga za NMG

Na ANITA CHEPKOECH na DAVID AJUNA June 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MUUNGANO wa Wanahabari nchini Kenya na Chama cha Wanahabari Afrika Mashariki kimekashifu kufungwa kwa runinga ya NTV Uganda na Spark kutokana na amri ya mkuu wa majeshi wa Uganda Jenerali Muhoozi Kainerugaba.
Vituo hivyo vya NMG vinavyopatikana Namuwongo na Hoteli ya Serana, Kampala vilivamiwa jana. Aidha, hadi sasa hatima ya magazeti na idhaa nyingine za NMG haijulikani likiwemo gazeti maarufu la Daily Monitor.
Vituo hivyo vya NMG vilivamiwa usiku wa manane wa kuamkia jana huku wafanyakazi wakisema hawakuruhusiwa kuingia kazini.
Runinga za NTV Uganda na Spark zilifungwa hivyo hazipeperushi habari zozote.
“NTV na Monitor zinafungwa kuanzia leo. Zote hazitafunguliwa tena bila idhini yangu,” akaandika saa saba na dakika saba usiku wa kuamkia Jumapili.
Kwenye chapisho jingine aliandika, “Hapa Uganda, siamini katika uhuru wa vyombo vya habari. Vyombo vya habari vinastahili kuongozwa na msingi wa mageuzi.”
Machapisho haya yanafuata vitisho ambavyo vilitolewa wiki jana ambapo Jenerali Muhoozi alidai mara si moja kwamba anasubiri idhini ya babake, Rais Yoweri Museveni kabla ya kufunga vyombo hivyo vya habari, ambavyo vimetoa ajira kwa mamilioni ya watu.
Nchini Uganda, NMG inamiliki NTV Uganda, The Daily Monitor, East Africa, Spark TV, 93.3 KFM, 90.4 Dembe FM, Gazeti la Ennyanda na Kampuni ya usafirishaji mizigo ya Nation Courier kati ya vyombo vingine vya habari.
Hakukuwa na maelezo kutoka kwa majeshi ya Uganda ama kwa Tume ya Mawasiliano ya Uganda kuhusu kufungwa kwa runinga hizo au amri yoyote ya kisheria.
 “Tunatoa wito kwa serikali ya Uganda ifuate sheria iwapo inaamini kuna sheria ambayo ilivunjwa.
“Tuko pamoja na wanahabari wenzetu wa Uganda,” akasema Rais wa Muungano wa Wanahabari Afrika Mashariki Eric Oduor.
 Baraza la Vyombo vya Habari Afrika Mashariki nalo lilisema uhasama kati ya vyombo vya habari na serikali katika ukanda huu unastahili kutafutiwa suluhu.
Baraza hilo lilishutumu serikali za ukanda huu kwa kutishia na kuwalenga wanahabari, tabia ambayo inaendelezwa na viongozi wanaoshikilia nyadhifa za juu serikalini.