Ripoti yaanika kaunti hatari kufanya biashara
RIPOTI ya Mdhibiti wa Bajeti imefichua kuwa kaunti 10, zikiwemo Nairobi, Mombasa, Machakos, Wajir na Garissa, ndizo zinazoongoza kwa kuchelewesha malipo kwa wanakandarasi na wauzaji wa bidhaa na huduma.
Ripoti hiyo inaonyesha kuwa wanakandarasi wengi wanaendelea kuteseka huku magavana wa sasa wakikataa kulipa madeni yaliyoachwa na watangulizi wao, hali inayohusishwa na uhasama wa kisiasa.
Kufikia Machi 31, 2026, kaunti zote 47 zilikuwa na madeni ambayo hazijalipa ya kima cha Sh156.84 bilioni.
Kati ya fedha hizo, zaidi ya Sh84 bilioni ni madeni ambayo yamekaa bila kulipwa kwa zaidi ya miaka mitatu.
Kaunti ya Mombasa, inayoongozwa na Gavana Abdulswamad Nassir, ndiyo iliyoongoza kwa kuwa na asilimia 98 ya madeni yake ambayo imechelewa kulipa kwa zaidi ya miaka mitatu.
Kaunti nyingine zilizoorodheshwa kuwa na sehemu kubwa ya madeni ya muda mrefu ni Wajir (asilimia 80), Nairobi (asilimia76), Mandera (asilimia75), Murang’a (asilimia 74), Kiambu (asilimia 67), Laikipia (asilimia 65), Embu (asilimia 65), Machakos (asilimia 54) na Garissa (asilimia 52).
Kwa upande mwingine, kaunti za Baringo, Bomet, Elgeyo Marakwet, Kericho, Kirinyaga, Kitui, Kwale, Lamu, Makueni, Marsabit, Nandi, Nyandarua na Nyeri zimekusanya madeni mengi chini ya tawala za magavana wa sasa.
Ripoti hiyo inaonyesha kuwa kucheleweshwa kwa malipo ya wanakandarasi sasa limekuwa tatizo sugu, huku baadhi yao wakifilisika, kufunga biashara au hata kuripotiwa kujitoa uhai kutokana na shinikizo za madeni kutoka kwa taasisi za kifedha.
Katika Kaunti ya Wajir, madeni ya zaidi ya miaka mitatu yanafikia Sh1.94 bilioni, ilhali yale yaliyolimbikiza ndani ya mwaka mmoja ni Sh488 milioni pekee.
Nairobi ndiyo inaongoza kwa kiwango kikubwa ambapo inadaiwa Sh81.13 bilioni. Kati ya fedha hizo, Sh61.6 bilioni ni madeni ya zaidi ya miaka mitatu, huku ya chini ya utawala wa sasa yakiwa sehemu ndogo ya salio hilo.
Katika Kaunti ya Murang’a, madeni ya zaidi ya miaka mitatu yanafikia Sh846.3 milioni, huku yale yaliyotokana na utawala wa sasa yakiwa Sh299.9 milioni.
Kiambu ina zaidi ya Sh3.56 bilioni za madeni ya zaidi ya miaka mitatu, huku Laikipia ikiwa na Sh852.1 milioni, Embu Sh830.3 milioni na Machakos Sh2.85 bilioni.
Garissa nayo ina madeni ya muda mrefu yanayofikia karibu Sh797.3 milioni.
Mdhibiti wa Bajeti, Bi Margaret Nyakang’o, alisema hali hiyo inaweka serikali za kaunti katika hatari kubwa kwani huenda zikashindwa kulipa madeni hayo kabla ya muda wao wa kuhudumu kumalizika.
Kwa mujibu wa Sheria ya Usimamizi wa Fedha za Umma ya Serikali za Kaunti ya mwaka 2015, serikali za kaunti zinapaswa kupatia kipaumbele malipo halali ambayo hayajalipwa katika bajeti ya mwaka unaofuata.
Ripoti hiyo pia inaonyesha kuwa madeni ya chini ya mwaka mmoja yanafikia Sh30 bilioni, yale ya kati ya mwaka mmoja na miwili ni Sh19.45 bilioni, huku ya kati ya miaka miwili na mitatu yakiwa Sh15.22 bilioni.
Aidha, Mdhibiti wa Bajeti alisema kaunti kadhaa hazikufuata ratiba zao za kulipa madeni hayo, huku Serikali ya Kaunti ya Kakamega ikikosolewa kwa kutowasilisha uchambuzi wa muda wa madeni yake kufikia Machi 31, 2026.