Habari za Kitaifa

Serikali yaondoa Wakenya Afrika Kusini baada ya kampeni ya chuki

Na NDUBI MOTURI July 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KUNDI la kwanza la Wakenya wanaotoroka mashambulizi ya kibaguzi dhidi ya wageni nchini Afrika Kusini liliwasili nchini jana asubuhi huku serikali ikiendelea na mpango wa kuwaokoa raia wake wanaotaka kurejea nyumbani.

Wizara ya Masuala ya Kigeni na Masuala ya Wakenya wanaoishi ng’ambo ilisema Wakenya 26 waliwasili na wengine 63 walitarajiwa kutua jana usiku na makundi mengine kuwasili Jumatano.

Katibu wa Idara ya Diaspora Roseline Njogu alisema waliofika ni kundi la kwanza katika operesheni kubwa ya kuwaondoa Wakenya wanaohisi maisha yao yako hatarini kutokana na mashambulizi hayo.

“Tunafanya kila tuwezalo kuhakikisha Wakenya wako salama. Watu 26 waliofika ni kundi la kwanza. Tunatarajia wengine 63 baadaye leo na kundi jingine kesho,” alisema.

Kwa mujibu wa Bi Njogu, zaidi ya Wakenya 200 wamejiandikisha kusaidiwa kurejea nchini baada ya serikali kuwaomba wale wanaohisi kutishiwa usalama wao wajitokeze.