Habari za Kitaifa

Maandamano yatikisa elimu, wanafunzi wakikosa kuenda shule

Na MERCY SIMIYU July 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MAELFU ya wanafunzi nchini wameendelea kupoteza muda muhimu wa masomo kutokana na kufungwa kwa shule kila kunapozuka maandamano ya kisiasa, huku wazazi wengi wakiamua kusalia na watoto nyumbani kwa hofu ya usalama.

Shule zilizo katika maeneo ya mijini ndizo zimeathirika zaidi, hasa zile zilizo karibu na maeneo ambayo waandamanaji hukabiliana na polisi.

Miongoni mwa shule hizo ni Moi Avenue Comprehensive School katikati mwa jiji la Nairobi, Jamhuri High School na St Brigid’s Public Primary School.

Shule nyingine katika kaunti za Machakos, Kiambu, Mombasa, Kisumu na Nakuru pia zimeripoti kusitisha masomo kila kunapoandaliwa maandamano kutokana na hofu ya usalama.

“Mimi sikuwapeleka watoto wangu shuleni licha ya serikali kusema ni siku ya kawaida ya kazi. Hatari ilikuwa kubwa mno,” alisema mzazi wa Nairobi, Nelly Koki.

Katika maandamano ya kuadhimisha Saba Saba, shule kadhaa zilisitisha masomo ya darasani.

Baadhi ziliwaagiza wazazi kuwa na watoto nyumbani, nyingine zikaendesha masomo mtandaoni huku baadhi zikiwapa kazi za kufanyia nyumbani.

Ingawa Wizara ya Elimu haikutoa agizo la kitaifa la kufunga shule, wasimamizi wengi wa shule walisema walichukua hatua hiyo kama tahadhari kutokana na hali ya usalama na changamoto za usafiri.

Huduma ya Kitaifa ya Polisi ilitangaza kuwa kutakuwa na ukaguzi mkali wa watu na magari katika barabara mbalimbali za Nairobi ili kuhakikisha amani inadumishwa.

Taarifa a zilionyesha shule ziliwafahamisha wazazi kuwa masomo yangeendelea kupitia kazi za nyumbani ili kuwatayarisha wanafunzi kwa mitihani ya mwisho wa muhula.

Hii si mara ya kwanza.

Wakati wa maandamano ya upinzani wa 2023 na yale ya kupinga Mswada wa Fedha wa 2024, shule nyingi zilifungwa kwa muda huku baadhi zikiahirisha kufunguliwa baada ya likizo ya katikati ya muhula.

Maandamano hayo pia yaligharimu maisha ya wanafunzi wa vyuo vikuu na shule, hali iliyoibua wasiwasi kuhusu usalama wa wanafunzi wakati wa misukosuko ya kisiasa.