Habari za Kaunti

Mombasa yaweka mfano bora wa maandamano yaliyojaa amani

Na BRIAN OCHARO July 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HUKU ulinzi mkali ukiwekwa sehemu nyingi nchini kwa hofu ya vurugu wakati wa maadhimisho ya Saba Saba, Mombasa iliendelea kujitokeza kama mfano wa jinsi maandamano yanavyoweza kufanyika kwa amani bila matumizi ya vitoa machozi, kukamatwa kwa waandamanaji au uharibifu wa mali.

Kwa mwaka wa pili mfululizo, waandamanaji katika jiji hilo la pwani waliandamana kwa utulivu, wakipinga dhana kwamba maandamano lazima yaambatane na vurugu, maafa na uharibifu wa mali.

Tofauti na ilivyoshuhudiwa katika maeneo mengine, hakukuwa na taarifa za watu kupigwa, kukamatwa au polisi kutumia vitoa machozi.

Aidha, hakukuwa na vizuizi vya barabarani katika njia kuu zinazoingia na kutoka katikati mwa jiji la Mombasa.

Biashara ziliendelea kama kawaida, magari ya uchukuzi wa umma yaliendelea na shughuli zake huku waandamanaji wakipita katika barabara kuu wakipaza sauti za kutetea demokrasia na uhuru.

Kamanda wa Polisi wa Kaunti Ndogo ya Mombasa Nicholas Chalulot, alisema maandamano ya amani hayawezekani bila maandalizi ya kina na mawasiliano ya karibu kati ya waandalizi na maafisa wa usalama.

“Maandamano ya amani yanaweza kuvamiwa na wahuni, hivyo huwa tupanga mapema na kuhakikisha polisi wapo kila mahali. Uwepo wao huwazuia wanaotaka kuvuruga maandamano,” alisema.

Aliongeza kuwa mazungumzo kati ya polisi na waandalizi hufanyika kabla na wakati wa maandamano ili kutatua tofauti zozote zinazojitokeza.

“Tunakubaliana, wakati mwingine hatukubaliani, lakini mwisho wa siku tunafikia mwafaka na maandamano huendelea kwa amani,” alisema.

Alisema pia maafisa wa polisi hupewa maelekezo ya kutowachokoza waandamanaji. “Wasipochokozwa, uwezekano wa vurugu hupungua sana,” aliongeza.

Kwa upande wake, mratibu wa Mtandao wa Mashirika ya Kijamii ya Pwani kuhusu Haki za Kibinadamu, Aisha Khamis, alisema mafanikio ya maandamano hayo huanza na maandalizi ya muda mrefu.

Kulingana naye, ujumbe unaotumwa kupitia WhatsApp na mitandao mingine ya kijamii huwa mmoja: watu wahudhurie na kudumisha amani, wasibebe silaha na wakumbuke kuwa lengo ni kufikisha ujumbe, si kupambana na polisi.

“Barabara si uwanja wa vita. Tunakuja kutoa ujumbe na kuwaenzi waliopigania nafasi ya kidemokrasia tunayofurahia leo,” alisema.

Naye mwanaharakati Lydia Adhiambo alisema waandalizi huwafahamisha polisi mapema kuhusu njia watakazotumia na maeneo ya kukusanyika, jambo ambalo limechangia kudumisha utulivu.