Wakulima wahimizwa kukumbatia nafaka zinazostahimili ukame
MABADILIKO ya tabianchi yameendelea kuathiri uzalishaji wa chakula nchini Kenya kutokana na mvua isiyotabirika, ukame wa mara kwa mara na ongezeko la joto.
Hali hii imepunguza mavuno ya mazao ya kawaida kama vile mahindi, hivyo wataalamu wanashauri wakulima kuanza kulima nafaka na mbegu zinazostahimili ukame ili kujenga mfumo wa kilimo unaoweza kuhimili mabadiliko ya hali ya hewa.
“Kuna nafaka ndogo ambazo zinahimili athari za tabianchi kama vile ukame na joto, na baadhi yanaweza kuwa kutumika badala ya mahindi,” anasema Dkt Ndungu Kabare, mtaalamu wa kilimo na mkulima kutoka Ruiru.
Kulingana na Dkt Kabare, mazao kama vile mtama, wimbi, teff, amaranth na chia yanahitaji maji kidogo, hukomaa haraka na yana misimu miwili ya mavuno kwa mwaka.

“Tofauti na mahindi, mazao haya yana uwezo mkubwa kustahimili vipindi virefu vya ukame bila kupungua sana kiuzalishaji,” anaelezea mtaalamu huyo.
Mbali na kustahimili mabadiliko ya tabianchi, nafaka hizi zina thamani kubwa ya lishe. Zina madini faafu kwa binadamu, vitamini, na antioxidants kwa kiwango cha juu zaidi kuliko baadhi ya nafakaa.
Hali kadhalika, nafaka hizo zina kiwango cha chini cha sukari kinachoingia haraka mwilini (glycemic index), hivyo zinafaa kwa watu wenye maradhi ya kisukari na unene kupita kiasi.
“Kwa upande wa biashara, soko la mazao haya linaendelea kukua kutokana na ongezeko la watumiaji wanaotafuta vyakula bora kiafya,” Dkt Kabare anasema.

Viwanda vya kusaga nafaka, watengenezaji wa vyakula vyenye mseto wa virutubisho, mikate na chakula cha mifugo, pia, vinahitaji malighafi hii, huku teff ikipata ikivutia masoko ya kimataifa.
Kulingana na Dkt Kabare, kupanua kilimo cha nafaka na mbegu zinazostahimili ukame kutasaidia Kenya kupunguza utegemezi wa mahindi, kuimarisha usalama wa chakula na kuongeza kipato cha wakulima.
Aidha, anasisitiza kuwa mafunzo, mbegu bora na uhamasishaji wa wakulima ni muhimu ili mazao haya yakubalike na kulimwa kwa kiwango cha juu nchini.