Wakazi Mbeere walia kuondolewa transfoma ‘baada ya kura’
WAKAZI wa eneo bunge la Mbeere North, Kaunti ya Embu, wamelalamikia kuondolewa kwa transfoma za umeme miezi minane tu baada ya serikali kuwaunganishia umeme kupitia mpango wa Last Mile Connectivity na Stima Mashinani.
Wakazi hao wanasema walipata umeme kwa mara ya kwanza wakati wa uchaguzi mdogo wa Novemba 27, 2025, lakini sasa wanahofia kurejea gizani baada ya Kampuni ya Kusambaza Stima Kenya (KPLC) kuanza kuondoa transfoma bila maelezo ya kina.
Faith Kithaka wa kijiji cha Muramba asema maafisa wa KPLC waliondoa transfoma katika eneo lao wiki mbili zilizopita na hawajairejesha.
Wakazi wanasema kuondolewa kwa transfoma hizo kumekatiza shughuli zao za kila siku na kuwarudisha katika maisha ya kutumia mishumaa na taa za mafuta.
“Tuliishi gizani kwa miaka mingi. Serikali ilituunganishia umeme wakati wa uchaguzi mdogo, lakini kabla hatujafaidika kikamilifu, transfoma zimeondolewa,” alisema Bi Kithaka.
Katika kijiji cha Njarange, hali ilikuwa sawa huku wakazi wakishuhudia maafisa wa KPLC wakiondoa transfoma nyingine.
Julius Njeru wa kijiji cha Rwanjeru alisema kukosekana kwa umeme kumeathiri biashara na masomo ya watoto.
“Biashara zimeathirika na watoto hawawezi kusoma usiku kwa sababu stima zimekatika,” alisema.
Baadhi ya wakazi walikumbuka jinsi viongozi wa serikali na wanasiasa wa chama cha UDA walivyozunguka eneo hilo wakati wa uchaguzi mdogo wakiahidi maendeleo iwapo wangemuunga mkono mgombea wa chama hicho.
“Tuliwapigia kura na tukaletewa umeme. Sasa miezi michache baadaye wanaondoa transfoma. Hii si haki,” alisema mkazi mmoja.
Wengine walidai kuwa transfoma hizo zinapelekwa Ol Kalou, ambako kutafanyika uchaguzi mdogo Julai 16, ili kuvutia wapigakura.
Wakazi walitishia kuandamana iwapo vifaa hivyo havitarejeshwa haraka.
Hata hivyo, Mbunge wa Mbeere North, Leo Wamuthende, alipuuza madai hayo akisema baadhi ya watu wanapotosha umma kwa maslahi ya kisiasa.
“Nimeona taarifa zinazodai serikali inaondoa transfoma katika Mbeere North. Madai hayo si ya kweli na yanalenga kupotosha wananchi,” alisema.
Alifafanua kuwa KPLC inaendesha mpango wa kawaida wa kukarabati transfoma, hasa zile za zamani, ili kuboresha uthabiti wa huduma ya umeme.
Meneja wa KPLC Kaunti ya Embu Vincent Okello, pia alikanusha madai kuwa transfoma hizo zinapelekwa Ol Kalou kwa sababu za kisiasa.
Alisema kampuni hiyo “haijihusishi na siasa” na kueleza kuwa baadhi ya transfoma ziliharibiwa na wahalifu huku nyingine zikiharibika kutokana na hitilafu za kiufundi.
“Katika Mbeere North na Runyenjes, transfoma tatu ziliharibiwa na ziliondolewa kupelekwa Nairobi kutengenezwa,” alisema.
Hata hivyo, baadhi ya wakazi walitilia shaka maelezo hayo wakisema baadhi ya transfoma zilizoondolewa ni mpya na hazikuwa na hitilafu zozote.
“Transfoma hazikuharibiwa wala kuvurugwa. Tunataka tuambiwe ukweli kuhusu zilikopelekwa,” alisema mkazi mwingine.