Habari

Matumaini tele KNH ikifanya upasuaji wa kihistoria wa saratani ya koo

Na HELLEN SHIKANDA July 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HOSPITALI ya Kitaifa ya Kenyatta (KNH) imeandika historia baada ya kufanikisha kwa mara ya kwanza nchini upasuaji wa kisasa usiohitaji kufungua kifua na tumbo kwa kiasi kikubwa ili kumtibu mgonjwa wa saratani ya koo, hatua inayowapa matumaini wagonjwa wengi.
Mnufaika wa upasuaji huo ni Joshua Wanzala, ambaye alikuwa akisumbuliwa na saratani ya koo Stage 2B.
Baada ya kufanyiwa upasuaji huo, sasa anaendelea kupata nafuu katika Kitengo cha Wagonjwa Mahututi cha KNH.
Joshua alisema matatizo yake yalianza mwaka jana aliposhindwa kumeza chakula na hata mate. Awali alidhani alikuwa na maambukizi ya kawaida, lakini vipimo vilibaini alikuwa na saratani ya koo.
Alihamishiwa KNH ambako alipokea vipindi 29 vya tibakemia.
Hata hivyo, matibabu yake yalikwama kwa muda baada ya mashine kuharibika.
Licha ya uvimbe kupungua, Joshua aliendelea kushindwa kula vizuri na uzani wake ukashuka kutoka kilo 80 hadi 40.
“Nilikuwa nakufa kwa njaa kwa sababu sikuweza kumeza chakula,” alisema.
Baadaye alifanyiwa upasuaji ulioongozwa na Dkt Joseph Mutie kwa ushirikiano na Dkt Obed Makori na madaktari wengine.
Badala ya kufungua kifua na tumbo kwa upasuaji mkubwa, madaktari walitumia vifaa maalumu na kamera kupitia matundu madogo.
Joshua alisema alishangaa kuona baada ya upasuaji alikuwa na majeraha madogo pekee na sasa anahisi mwenye nguvu zaidi, ingawa bado hajaanza kula kawaida.
Amesema tayari ametumia takriban Sh800,000 kugharamia matibabu, lakini ameelezwa kuwa Mamlaka ya Afya ya Kijamii (SHA) itagharamia gharama za upasuaji huo.
Kwa mujibu wa Dkt Mutie, upasuaji huo hufanywa kwa wagonjwa ambao saratani yao haijasambaa sana mwilini. Alisema faida zake ni kupunguza maumivu, kupunguza kupoteza damu, kuharakisha kupona na kuwapa madaktari mwonekano mzuri zaidi wakati wa upasuaji.
Katika upasuaji huo, koo huondolewa kabisa na tumbo hubadilishwa kuwa mrija unaounganishwa na sehemu iliyobaki ya koo ili mgonjwa aweze kula tena.
Dkt Mutie alisema wagonjwa hulazimika kula chakula kidogo mara nyingi na vyakula vyenye virutubisho vingi, lakini wanaweza kuendelea kuishi maisha yenye ubora mzuri.