Kupata huduma muhimu bado ni changamoto licha ya serikali kuanzisha vitengo vipya vya utawala 2023
LICHA ya serikali kuanzisha vitengo vipya vya utawala nchini tangu mwaka 2023 kwa lengo la kupeleka huduma karibu na wananchi, kuimarisha usalama na kuboresha uratibu wa shughuli za serikali, uchunguzi umebaini baadhi ya vitengo hivyo bado havijaanza kufanya kazi kikamilifu.
Sababu kuu zinazochelewesha utekelezaji ni ukosefu wa fedha, kuchelewa kuajiri machifu na manaibu wao, pamoja na ukosefu wa ofisi na miundombinu muhimu.
Maeneo yaliyoathirika zaidi ni Kaskazini Mashariki na Bonde la Ufa, ambako vitengo vingi vilianzishwa ili kukabiliana na changamoto za usalama.
Katika eneo la Kaskazini Mashariki pekee, angalau tarafa saba, kata 26 na kata ndogo 38 bado havijaanza kutoa huduma.
Kaunti ya Wajir inaongoza kwa kuwa na vitengo 40 visivyofanya kazi, ikifuatiwa na Garissa ikiwa na 19 na Mandera 12.
Wakazi wanasema changamoto za usalama, migawanyiko ya koo na uhaba wa watumishi zimekwamisha utekelezaji.
Garissa kwa mfano, baadhi ya wakazi bado husafiri zaidi ya kilomita 150 kupata huduma muhimu kama vitambulisho vya kitaifa na vyeti vya kuzaliwa.
Kamishna wa Kanda ya Kaskazini Mashariki, Bw John Otieno, hata hivyo alisema mchakato unaendelea, akibainisha kuwa machifu na manaibu wao wanaendelea kuajiriwa huku manaibu wa makamishna wa kaunti tayari wakipelekwa katika maeneo mengi mapya.
Kaunti ya Turkana imeonyesha mafanikio na changamoto kwa pamoja. Vitengo vipya kama Lokichogio, Aroo, Lokiriama na Suguta vimechangia kuimarisha usalama katika baadhi ya maeneo ya mpakani, ingawa wizi wa mifugo, ukosefu wa magari ya doria na barabara mbovu bado vikitatiza utoaji wa huduma.
Katika mpaka wa Kenya na Sudan Kusini, wakazi wanasema hali ya amani imeimarika tangu kuanzishwa kwa vitengo hivyo mwaka 2024, huku kamati za amani na usimamizi wa rasilimali zikisaidia kuzuia migogoro.
Katika Kaunti ya Kilifi, Tarafa ya Chasimba ndiyo pekee inayokaribia kuanza kufanya kazi kikamilifu, huku maeneo mengine kama Kitsoeni na Mwakambi yakiwa bado hayana machifu wala ofisi.
Hali kama hiyo inashuhudiwa Taita Taveta ambako baadhi ya maeneo yanasubiri maafisa kupelekwa licha ya mahojiano kukamilika.
Kaunti za Homa Bay na Kisumu pia zina vitengo vipya ambavyo bado haviwezi kutoa huduma zote za serikali kutokana na ukosefu wa watumishi na miundombinu.
Wakazi wengi bado hulazimika kusafiri hadi makao makuu ya kaunti ndogo kupata huduma za usajili wa vitambulisho, vyeti vya kuzaliwa na huduma za polisi.
Hata hivyo, Busia, baadhi ya wakazi wanasema vitengo vipya vimepunguza gharama na muda wa kupata huduma za serikali.
Lakini katika maeneo jirani ya Mumias West, vituo vipya vya polisi bado havijaanza kufanya kazi licha ya fedha kutumika kujenga miundombinu hiyo.
Huko Samburu, zaidi ya miezi sita baada ya kutangazwa kwa kaunti ndogo mpya, utekelezaji bado umekwama kutokana na ukosefu wa fedha.