Habari

Mahakama yazimia marasta bangi, yataka mdahalo wa kitaifa kuhusu Wakenya wote

Na JOSEPH WANGUI July 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MAKAHAMA Kuu imetupilia mbali kesi iliyowasilishwa na Chama cha Warastafari Kenya iliyotaka wanachama wake waruhusiwe kulima, kumiliki na kutumia bangi kama sehemu ya ibada yao.

Jaji Bahati Mwamuye alisema walalamishi walishindwa kuthibitisha kuwa sheria za sasa zinakiuka haki zao za kikatiba.

Pia alisema hawakufuata utaratibu uliowekwa kisheria wa kuomba leseni ya kutumia dawa hizo kabla ya kuwasilisha kesi mahakamani.

“Si suala linalowahusu Warastafari pekee, bali ni mjadala wa kitaifa unaowahusu Wakenya wote. Tunahitaji mazungumzo ya wazi kuhusu matumizi ya bangi na mwelekeo ambao taifa linapaswa kuchukua,” akasema Jaji Mwamuye.

Hata hivyo, mahakama imesema ni wakati wa Wakenya kuanzisha mjadala kuhusu sera ya nchi dhidi ya bangi.

Kesi hiyo iliwasilishwa mnamo 2021 ikipinga baadhi ya vipengele vya Sheria ya Kudhibiti Dawa za Kulevya ambayo inaharamisha bangi.

Warastafari walidai bangi ni sakramenti takatifu inayotumika katika ibada, kutafakari na mikutano ya kiimani.

Kwa hivyo sheria hiyo inakiuka haki zao za kidini, usawa na heshima.

Hawakutaka bangi ihalalishwe kwa kila mtu, bali walitaka Warastafari wasishtakiwe wanapotumia au kushiriki kilimo cha bangi katika nyumba zao au maeneo maalumu ya ibada.

Kwa upande wake, Mwanasheria Mkuu alipinga ombi hilo akisema sheria hiyo inalenga kulinda afya na usalama wa umma na inatumika kwa Wakenya wote bila ubaguzi.

Mamlaka ya Kitaifa ya Kupambana Mihadarati (NACADA) pia iliambia mahakama kuwa, bangi ina madhara yaliyothibitishwa kiafya na kutoa idhini kwa kundi moja kungevuruga utekelezaji wa sheria.

Mahakama ilikubaliana kuwa dini ya Rastafari inalindwa na Katiba. Hata hivyo, jaji alisema ushahidi uliotolewa na walalamishi wenyewe ulionyesha kuwa baadhi ya Warastafari wanaabudu bila kutumia bangi.