Mkutano mkubwa wa Sifuna Bungoma wachemsha Magharibi Didmus naye akidaiwa kupanga wake
UMAARUFU unaozidi kuongezeka wa Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna umeibua ushindani mkali wa kisiasa katika eneo la Magharibi, huku viongozi wanaounga mkono serikali wakizidisha juhudi za kupunguza ushawishi wake.
Bw Sifuna anatarajiwa kuongoza mkutano mkubwa wa kisiasa katika uwanja wa Posta, Bungoma mnamo Julai 26.
Inatarajiwa kuwa baadhi ya wazee wa jamii ya Waluhya watamtawaza Bw Sifuna kuwa kinara mpya wa kisiasa wa eneo hilo na kumpa baraka za kuwania urais mnamo 2027.
Kabla ya mkutano huo, Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya anatarajiwa kuwa mwenyeji wa Bw Sifuna na viongozi wenzake wa Linda Mwananchi mjini Kitale Julai 16.
Kaunti za Bungoma na Trans Nzoia ni nyumbani kwa jamii ya Bukusu, ambako Sifuna anatoka.
Jamii hiyo pia imewahi kuwatoa viongozi mashuhuri kama aliyekuwa Makamu wa Rais Wamalwa Kijana na mwanasiasa marehemu Masinde Muliro ambaye alipigania mfumo wa vyama vingi.
Duru zinaarifu kuwa Mbunge wa Kimilili Didmus Barasa anapanga kufanya mkutano sambamba mjini Bungoma siku hiyo hiyo Bw Sifuna anatarajiwa mjini humo.
Bw Barasa, ambaye ametangaza kuwa atagombea ugavana wa Bungoma kwa tiketi ya UDA mnamo 2027, hakujibu simu wala ujumbe alipotafutwa kuthibitisha taarifa hizo.
Mabw Barasa na Sifuna wamekuwa wakirushiana cheche katika mikutano ya hadhara na mazishi, hali inayozua hofu kwamba mikutano yao kufanyika siku moja kunaweza kuzua ghasia.
Aliyekuwa Mbunge wa Kanduyi Wafula Wamunyinyi amelaani kile alichokitaja kuwa kampeni ya kupinga Sifuna inayoendeshwa na baadhi ya viongozi wa Mulembe.
“Ninawasihi watu wetu wajitokeze kwa wingi kumpokea mwana wetu Sifuna. Katika ziara za upinzani zilizopita kulikuwa na njama za kuvuruga mikutano yetu, na sasa tuna taarifa kuwa kuna mipango kama hiyo dhidi ya ziara ya Linda Mwananchi ila wananchi tayari wameamua,” alisema.
Uhasama kati ya Bw Sifuna na Barasa umejitokeza mara kadhaa katika hafla za umma.
Katika mazishi ya Patrick Wangamati, babake aliyekuwa Gavana wa Bungoma Wafula Wangamati, Bw Barasa aliondoka na umati mkubwa baada ya kuhutubia waombolezaji huku Bw Sifuna akimshutumu kwa kuwahonga wananchi.
“Anapoona ninasimama kuhutubu, huondoka na kuwapanga watu kwenye foleni kuwapa Sh200. Bungeni hupigia kura nyongeza ya ushuru ili wananchi waumie, halafu anarudi kuwagawia pesa,” akasema Bw Sifuna.
Bw Barasa baadaye alijibu kwa mzaha akidai marehemu Wangamati alimjia kwenye ndoto na kumshukuru kwa kuwapa waombolezaji fedha.
Katika mazishi ya nduguye Mbunge wa Bumula Wanami Wamboka Julai 5, Bw Sifuna alisisitiza Barasa azungumze mwisho ili asiondoke na waombolezaji.
Hata hivyo, Bw Barasa alitumia nafasi hiyo kuwashutumu viongozi wa Linda Mwananchi na kuwaita wachoyo. Baadaye kulitokea mzozo kati yake na Mbunge wa Kabuchai Majimbo Kalasinga, kabla ya Bw Barasa kufupisha hotuba yake na kuondoka akiwa ameandamana na umati mkubwa.
Iwapo mikutano yote miwili itafanyika Julai 26, huenda hali ya kisiasa Bungoma ikawa na taharuki zaidi, hasa wakati ambapo kumekuwa na visa vya makundi ya wahuni kuvuruga mikutano ya kisiasa.
Licha ya Bw Sifuna kuwa mzaliwa wa Bungoma, viongozi wanaomuunga mkono kiongozi wa Ford Kenya Moses Wetang’ula wanaendelea kusisitiza kuwa bado hajakomaa kuwania urais.
Kati ya viongozi waliochaguliwa Bungoma, ni Mbunge wa Bumula Wanami Wamboka na mwenzake wa Kabuchai Majimbo Kalasinga pekee waliotangaza wazi kumuunga mkono katibu huyo wa zamani wa ODM.
Gavana wa Bungoma Ken Lusaka, ambaye anaratibu kampeni za Rais William Ruto Magharibi, amesema eneo hilo linafaa kulenga kutoa rais mnamo 2032 badala ya 2027.
“Wakenya wanaweza kukushawishi ugombee urais, lakini siku ya kura wakakuacha peke yako,” alisema.
Wakati huo huo, Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula ameongeza mikutano ya mashinani na programu za uwezeshaji katika Magharibi, hatua inayotafsiriwa kama juhudi za kukabiliana na ushawishi unaoongezeka wa Sifuna.