Upinzani na serikali waanza kuhofia umaarufu wa Linda Mwananchi
MWANZONI, wengi walichukulia vuguvugu la Linda Mwananchi kama kundi jingine ambalo lingemezwa na miungano ya kisiasa inayobadilika kila mara nchini.
Hata hivyo, hali imebadilika.
Leo hii, serikali ya Rais William Ruto pamoja na muungano wa upinzani unaoongozwa na Kalonzo Musyoka na Rigathi Gachagua wanalitazama kama nguvu mpya inayoweza kuathiri matokeo ya uchaguzi mkuu wa 2027.
Matokeo ya hivi punde ya utafiti wa kura ya maoni uliofanywa na Infotrak yanaonyesha kuwa vuguvugu hilo limeongeza ushawishi wake kisiasa.
Kulingana na utafiti huo, kiongozi wa Wiper Musyoka angepata asilimia 13 ya kura ikiwa uchaguzi ungefanyika leo, huku kinara wa Linda Mwananchi Edwin Sifuna akiwa sawa na Fred Matiang’i wa Jubilee kwa asilimia 12.
Kwa mwanasiasa ambaye ameibuka hivi majuzi kama sura ya vuguvugu hilo, kiwango hicho cha uungwaji mkono kimebadili hesabu za kisiasa nchini.
Wachambuzi wanasema Sifuna sasa anaungwa mkono kwa kiwango ambacho hakiwezi kupuuzwa na Rais Ruto wala upinzani hauwezi kudhani kwamba kura zake zitahamia moja kwa moja kwa mgombea wao wa urais.
Hali hiyo imefanya Linda Mwananchi kujikuta ikikosolewa na pande zote mbili za kisiasa.
Akizungumza katika Ikulu Jumatatu, Rais Ruto aliwataka Wakenya kukataa upinzani na kumpa muhula wa pili.
“Wao ni hatari kubwa kwa nchi yetu. Hawana ajenda ya kuipeleka Kenya mbele, wanataka kuturudisha nyuma,” alisema.
Rais aliwashutumu wapinzani kwa kukosa mawazo mapya na kuendelea kurejelea sera ambazo tayari zilishindwa.
Ingawa hakulitaja moja kwa moja vuguvugu la Linda Mwananchi, kauli yake ilijiri wakati ambapo linaendelea kupata umaarufu kote nchini.
Kwa upande wake, Sifuna amesema serikali imeingiwa na hofu kutokana na ushawishi unaoongezeka wa vuguvugu hilo.
“Kila Mkenya anaweza kuona kwamba Linda Mwananchi imewashtua watu walio madarakani. Wanaamini njia pekee ya kutukabili ni kutumia vurugu, lakini hatutatishwa. Lazima nchi hii iokolewe,” alisema baada ya shughuli za vuguvugu hilo kuvurugwa Kisumu na Nyahururu.
Mchambuzi wa siasa Arnold Maliba anasema wengi walikosea kuchukulia Linda Mwananchi kama mshirika mwingine wa kisiasa.
Anasema kundi hilo limekuwa likiweka shinikizo kwa serikali na pia kwa upinzani kwa wakati mmoja.
Kulingana naye, nguvu yake kubwa si siasa za ukabila bali ajenda ya utawala bora, uwajibikaji, kuheshimu Katiba na ushiriki wa wananchi katika maamuzi.
“Lengo lake si kubadili tu aliye madarakani, bali kubadili namna siasa zinavyofanywa nchini,” anasema.
Anasema pia vuguvugu hilo limevuka mipaka ya vijana pekee.
Mbali na Sifuna na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, sasa limevutia wanafunzi, wataalamu, wafanyakazi, wastaafu na hata viongozi wa zamani wa mapambano ya demokrasia akiwemo Gavana wa Siaya James Orengo.
Aidha, limeanza kujijenga katika maeneo ambayo kwa muda mrefu yalikuwa ngome za vyama vikuu vya kisiasa, ikiwemo Nyanza, Nairobi, sehemu za Magharibi na Pwani.
Ukuaji huo umeanza kuwatia wasiwasi viongozi wa muungano wa upinzani.
Wiki iliyopita, Bw Gachagua alimuonya Gavana wa Murang’a Irungu Kang’ata dhidi ya kuwaalika viongozi wa Linda Mwananchi kufanya kampeni Ol Kalou kabla ya uchaguzi mdogo.
“Nimesikia Irungu Kang’ata akisema ataleta Linda Mwananchi Ol Kalou. Asilete kiherehere huko, si lazima,” alisema.
Kwa miezi kadhaa, upinzani umekuwa ukijaribu kupata mgombea mmoja wa urais kati ya Kalonzo Musyoka na Fred Matiang’i.
Hapo awali kulikuwa na mazungumzo kwamba Sifuna angeweza kuwa mgombea mwenza.
Lakini matokeo ya Infotrak yamebadili hali hiyo.
Mbunge wa Embakasi Kaskazini James Gakuya anasema Sifuna sasa ni mwanasiasa ambaye hawezi kupuuzwa.
“Sifuna ni nguvu kivyake. Uchaguzi ni mchezo wa nambari. Hakuna anayeweza kumpuuza,” alisema.
Kwa mujibu wa Gakuya, Sifuna bado ana uwezo wa kuvutia kura Nyanza, Magharibi, Pwani na Nairobi, jambo linalompa nguvu katika mazungumzo ya kisiasa.
Hata hivyo, Seneta wa Nandi Samson Cherargei anaamini bado hana miundo na fedha za kutosha kuwania urais.
“Kama ni kijana mwenye hekima, abaki kuwa Seneta wa Nairobi na ajenge nguvu zake polepole. Hana rasilimali wala chama cha kisiasa cha kutosha kuendesha kampeni za urais,” alisema.
Mchambuzi John Anditi anakubaliana naye akisema ushindi wa urais unahitaji fedha nyingi, maajenti wa uchaguzi, chama chenye mizizi kote nchini na muungano mpana wa kisiasa.
Lakini Geoffrey Mboya anaonya kuwa si lazima vuguvugu lishinde uchaguzi ili libadilishe siasa za nchi.
Anasema linaweza kubadili mjadala wa kitaifa, kuathiri mazungumzo ya miungano na kuvutia wapigakura ambao hawakuwa wakishiriki siasa.