Habari za Kitaifa

Ajabu bunduki ya jaji Muchelule kuhusishwa na ujambazi Nairobi, Kiambu na Kilifi

Na KAMORE MAINA July 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

BUNDUKI iliyoibwa kutoka kwa Jaji wa Mahakama ya Rufaa Aggrey Muchelule mnamo 2025 imehusishwa na uvamizi dhidi ya wateja wa mkahawa mmoja eneo la Westlands wiki iliyopita.

Silaha hiyo pia imehusisha na visa vya uhalifu katika kaunti za Nairobi, Kiambu na Kilifi.

Jumanne jioni, Jaji Muchelule aliwaambia polisi kwamba aligundua bunduki yake aina ya Beretta 92 ilikuwa imeibwa baada ya maafisa wa upelelezi kumpigia simu na kumfahamisha kuwa silaha hiyo imepatikana eneo la Joska, Kaunti ya Machakos.

Bunduki hiyo ilipatikana nyumbani kwa mshukiwa wa ujambazi ambaye polisi wanaamini alikuwa miongoni mwa watu walionaswa na kamera za CCTV wakiwapora wateja wa mkahawa wa Chaii Wali Café Westlands. Aliwapora simu, fedha na vitu vingine vya thamani.

Mshukiwa huyo aliuawa kwa kupigwa risasi na polisi Jumatatu baada ya kufyatuliana risasi na maafisa katika nyumba ya mpenzi wake huko Joska.

Kamanda wa Polisi wa Joska Peter Gichohi alisema mshukiwa alikuwa amejificha eneo hilo tangu kisa cha Chaii Wali Café, huku polisi wakiendelea kuwatafuta washukiwa wengine watatu waliotoroka.

Maafisa wa Idara ya Upelelezi Nchini (DCI) kutoka makao makuu na kituo cha polisi cha Matungulu walimkabili mshukiwa huyo, ambaye inadaiwa alianza kuwafyatulia risasi badala ya kujisalimisha.

DCI ilisema walipata bunduki hiyo, risasi nne za milimita tisa na simu tatu za mkononi.

Baada ya kuchunguza nambari ya usajili wa bunduki hiyo, ilibainika kuwa ilitolewa kwa Jaji Muchelule mnamo 2018.

Jaji huyo aliwaambia maafisa wa DCI kuwa baada ya kupokea simu kuhusu kupatikana kwa bunduki hiyo, alikimbia nyumbani kwake kuangalia kama bado ilikuwa salama, lakini hakuiona.

Katika taarifa yake kwa polisi, alisema alipokabidhiwa bunduki hiyo mnamo 2018 alikuwa amepewa risasi 15. Hii inaonyesha kuwa angalau risasi 11 tayari zimetumika.

Uchunguzi unaonyesha bunduki hiyo pia ilitumika katika tukio la ujambazi wa kutumia nguvu huko Mtwapa, Kaunti ya Kilifi, Februari mwaka huu.