Mke mwenza aliyeuguza mume ashinda kesi ya urithi wa Sh200 milioni
MAHAKAMA Kuu ya Mombasa imeamua kwamba, katika hali za kipekee, talaka inaweza kuchukuliwa kuwa ilitokea pale ambapo ndoa imekoma, kwa kuzingatia vitendo vya wanandoa ambao wameendelea na maisha yao tofauti hata kama hakuna amri rasmi ya talaka.
Mahakama ilisema ndoa inapaswa kuzingatia hali halisi ya maisha ya wahusika na kwamba ndoa inaweza tu kuendelea kuwepo kwa muda ambao wanandoa wote wanakubali kuendelea nayo.
Kulingana na mahakama, kushikilia vinginevyo kunaweza kuifanya ndoa ionekane kama aina ya kifungo gerezani na kukiuka haki ya kikatiba ya ridhaa ya hiari ya kuingia katika ndoa.
Uamuzi huo ulitolewa katika mzozo wa urithi wa mali yenye thamani ya zaidi ya Sh200 milioni kufuatia kifo cha Prem Lal Ramnath mnamo Novemba 24, 2019.
Mzozo uliwahusisha Bi R.B, aliyedai kuwa mjane wa marehemu, dhidi ya Bi A.G na watoto wake, V.L na Y.G.
Bi R.B aliwasilisha cheti kilichoonyesha kuwa alifunga ndoa na marehemu mwaka 1999 Mombasa na baadaye akaomba barua za usimamizi wa mirathi.
Alisema aliishi na marehemu kwa karibu miaka 20, akimsaidia katika biashara zake na kumhudumia wakati wa ugonjwa.
Pia alitoa figo moja mwaka 2012 ili kuokoa maisha ya marehemu.
Hata hivyo, Bi A.G na watoto wake walipinga mchakato huo, wakidai kwamba ndoa ya Kihindu kati ya Bi A.G na marehemu haikuwahi kuvunjwa, hivyo marehemu hangeweza kufunga ndoa nyingine kihalali.
Pia walidai kuwa Bi R.B alificha taarifa muhimu na alihusika katika udanganyifu wa kupata usimamizi wa mali.
Hata hivyo, ushahidi ulionyesha kuwa Bi A.G alihamia Canada mwaka wa 2001 na hakurejea Kenya hadi baada ya kifo cha marehemu mwaka 2019.
Pia ilikubaliwa kuwa marehemu aliishi na Bi R.B wakati wa kifo chake.
Mahakama ilibaini kuwa Bi A.G na marehemu walikuwa wameishi mbali kwa miaka mingi, huku Bi R.B akiwa ndiye aliyemhudumia marehemu wakati wa ugonjwa wake.
Mahakama ilikataa kubatilisha ndoa ya Bi R.B na marehemu, ikisema alikuwa mke wake na alikuwa na haki ya kuomba urithi bila kuhitaji ridhaa ya watoto wa marehemu.
Mahakama pia ilikataa madai kwamba Bi R.B alitoa figo kwa malipo, ikisema hakuna ushahidi wa malipo hayo na kwamba madai hayo yalilenga kuchafua sifa yake.
Pia ilikosoa walalamishi kumtaja kwa dharau kutokana na kazi yake ya awali ya kusakata densi, ikisema mtazamo huo unaonyesha ubaguzi wa kitabaka.
Kwa kuzingatia hali halisi ya uhusiano huo, mahakama ilisema si haki kwa mwenzi anayemwacha mwenzake kwa muda mrefu na kuishi maisha ya kujitegemea kurejea baadaye na kudai mali ambayo huenda mwenzi mwingine aliitafuta na kuijenga wakati wa kutokuwepo kwake.