Madini muhimu yazidi kuvutia wawekezaji Pwani
WAWEKEZAJI mbalimbali wamezidisha juhudi za kufaidi kutokana na madini mengi Pwani yanayotegemewa ulimwenguni kutengeneza vifaa vya kielektroniki.
Miongoni mwao ni kampuni ya Maboka Mining, ambayo iliwasilisha ripoti ya uchunguzi wa athari za kimazingira kwa Mamlaka ya Kitaifa ya Kusimamia Mazingira (NEMA) hivi majuzi.
Kampuni hiyo inalenga kuchimba madini ya coltan, beryllium na cerium katika sehemu ya Mbuga ya Kitaifa ya Kora iliyo Kaunti ya Tana River.
Madini hayo muhimu hutumiwa katika viwanda vya kutengeneza vifaa vya kisasa ikiwemo vyombo vya kielektroniki, ndege, silaha za kijeshi, vifaa vya kimatibabu, miongoni mwa mengine.
Kampuni hiyo imependekeza kujenga kiwanda cha uchimbaji na usafishaji wa madini ghafi kwa gharama ya karibu Sh461 milioni.
“Licha ya manufaa ya mpango huo, kuna pia uwezekano wa athari kwa mazingira,” ripoti hiyo inasema.
“Kutokana na uwepo wa madini katika eneo hilo, kumekuwa na uchimbaji unaofanywa na wachimbaji wadogowadogo wa madini hapo awali kwa njia inayoharibu ardhi.
Shughuli za uchimbaji zinafaa kufanywa kwa muda mfupi iwezekanavyo kisha ardhi irudishwe katika hali yake halisi,” ripoti ikaongeza.
Katika Kaunti ya Kilifi, kampuni ya Leibra Investments Limited imewasilisha pendekezo la kuchimba madini ya manganese.
Ombi hilo lilichapishwa kwenye gazeti rasmi la serikali na Waziri wa Madini, Uchumi wa Baharini na Masuala ya Ubaharia, Bw Hassan Joho, mnamo Ijumaa wiki iliyopita.
Wananchi walipewa siku 42 kuwasilisha pingamizi lolote kwa Waziri.
Manganese hutumiwa sana katika uzalishaji wa chuma, lakini katika miaka ya hivi majuzi, madini hayo yamethaminiwa zaidi ulimwenguni kwa matumizi katika utengenezaji wa betri za magari ya elektroniki.
Kwa mujibu wa ripoti za biashara ya madini hayo, soko la manganese ulimwenguni linatarajiwa kukua kutoka dola bilioni 32.98 (Sh4.3 trilioni) mwaka huu hadi dola bilioni 45.35 (Sh5.9 trilioni) mwaka wa 2032.
Mpango huo wa Kilifi ukiidhinishwa, utaongezea juhudi za Kenya kuchimba madini hayo kutoka Lali Hills, Kaunti ya Tana River.
Wizara ya Madini ilikuwa imetangaza wito kwa wawekezaji kuwasilisha mapendekezo ya uchimbaji Lali Hills mapema mwaka huu, na kueleza kuwa madini ya manganese yamekuwa yakichimbwa kwa kiwango kidogo Kilifi.
Serikali imekuwa ikiendeleza juhudi za kurekebisha sekta ya madini ili kuvutia uwekezaji huku ikiimarisha usalama, utunzaji mazingira na faida kwa jamii pamoja na nchi.
Katika hotuba zake, Rais William Ruto amekuwa akisisitiza kwamba makubaliano yoyote ya uchimbaji madini lazima yahakikishe utengenezaji unafanywa humu nchini, tofauti na awali ambapo madini ghafi yalikuwa yakichimbwa na kupelekwa nje ya nchi.
Hata hivyo, mpango mkubwa zaidi wa uchimbaji madini katika Mrima Hill, Kaunti ya Kwale, umekumbwa na misukosuko.
Akiongea pembezoni mwa mkutano wa G7 nchini Ufaransa, Rais Ruto alisema kulikuwa na mpango wa makubaliano kati ya Kenya na Marekani wa kuchimba na kutumia madini ya Mrima.
Kundi la wanaharakati lilielekea mahakamani kuomba mpango huo usitishwe, likidai kuwa makubaliano hayo yalijadiliwa bila kushirikisha umma.
Eneo hilo lina madini ya niobium na mengine ambayo ni muhimu kwa teknolojia, ulinzi na viwanda yanayokadiriwa kuwa na thamani ya karibu dola bilioni 62 (Sh9.7 trilioni).