Habari

Walimu wapokea mafunzo ya kugundua dalili za itikadi za ugaidi mapema

Na KNA July 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

WALIMU kadha katika eneo la Pwani wamepokea mafunzo kuhusu jinsi ya kukabili itikadi kali.

Mafunzo hayo yanayotolewa na Wizara ya Elimu na Kituo cha Kitaifa cha Kuzuia Ugaidi (NCTC) yalihusisha walimu karibu 40 kutoka shule mbalimbali za umma ili waweze kutambua mapema na kuepusha dalili za uenezaji itikadi kali shuleni, ambazo husababisha vijana kusajiliwa katika makundi ya kigaidi.

Mkuu wa Mawasiliano katika NCTC, Bw Charles Opiyo, alisema ni muhimu walimu kupokea mafunzo hayo kwa sababu wana uhusiano wa moja kwa moja na wanafunzi.

“Walimu ndio walezi wa vijana hawa na wao huwa na uhusiano wa karibu zaidi na wanafunzi kuliko mtu yeyote mwingine katika mfumo wa elimu.

Kutokana na kuwa vijana wadogo ndio hulengwa zaidi na makundi ya kigaidi, kuwapa walimu ujuzi huu kutawawezesha kutambua mabadiliko ya tabia mapema na huenda wakafanikiwa kuokoa maisha,” akasema Bw Opiyo.