Ombi la Odemba latimia, KBC kupeperusha WAFCON bila malipo
AZMA ya kocha wa Harambee Starlets, Beldine Odemba ya Shirika la Utangazaji Kenya (KBC) kupata haki za kupeperusha moja kwa moja mechi zote za Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wanawake (WAFCON) 2026 kupitia KBC Channel 1 imetimia.
Mashindano hayo yataandaliwa nchini Morocco kuanzia Julai 26 hadi Agosti 16.
Kulingana na kiongozi mmoja wa KBC, aliyeomba kutotajwa, alithibitisha maendeleo hayo kwa Taifa Spoti jana.
“Ni kweli, mechi zote za WAFCON zitaonyeshwa kupitia KBC,” alisema kiongozi huyo.
Hatua hiyo inawapa Wakenya fursa ya kufuatilia timu ya taifa ya Kenya ya Soka ya Wanawake ya Harambee Starlets wanaporejea kwenye fainali za bara kwa mara ya kwanza tangu mwaka wa 2016.
Uthibitisho huo umejiri siku chache baada ya Odemba kumwomba Rais William Ruto kuhakikisha KBC inapata haki za kupeperusha mashindano hayo ili Wakenya waweze kuitazama na kuipa timu ya taifa ya wanawake sapoti.
Kocha huyo alitoa ombi hilo Julai 14 wakati wa hafla ya kiamsha kinywa na kuaga timu iliyoandaliwa Ikulu kabla ya kikosi hicho kuelekea Ufaransa kwa kambi ya maandalizi.
“Mheshimiwa Rais, ninaomba uhakikishe KBC inapata haki za kuonyesha WAFCON ili Wakenya waweze kutazama na kuisapoti timu ya taifa ya wanawake katika mashindano yote,” alisema Odemba.
Katika hafla hiyo pia, Odemba aliitaka serikali kuwania haki za kuandaa WAFCON ya mwaka 2028, akisema miundombinu inayojengwa kuelekea fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027 itaiweka Kenya katika nafasi nzuri ya kuandaa mashindano hayo ya wanawake.
Aliongeza: “Kenya itaandaa AFCON 2027, hivyo miundombinu itakuwa tayari. Baada ya WAFCON ya mwaka huu kutakuwa na nyingine mwaka 2028. Tunaomba mtusaidie tuwe wenyeji wa mashindano hayo.”
Kwa sasa, kikosi cha wachezaji 24 kimeweka kambi mjini Miramas, kusini mwa Ufaransa, kikijiandaa kabla ya kuelekea Morocco baadaye wiki hii.
Kenya imepangwa Kundi A pamoja na wenyeji Morocco, Senegal na Algeria.
Starlets itaanza kampeni yake dhidi ya Morocco Jumapili katika Uwanja wa Moulay El Hassan mjini Rabat, kabla ya kuvaana na Senegal Julai 30 kwenye uwanja huo. Mechi ya mwisho ya makundi itakuwa dhidi ya Algeria Agosti 3 katika Uwanja wa Al Medina, Rabat.
Mashindano ya WAFCON pia yatatumika kama hatua ya kufuzu kwa Kombe la Dunia la Wanawake la FIFA 2027 nchini Brazil, huku timu zitakazofika nusu fainali zikifuzu moja kwa moja.