NI HISTORIA: Sababu za Kenya kutuzwa uandalizi wa mbio kubwa zaidi duniani
HISTORIA pevu ya Kenya katika riadha, ongezeko kubwa la mashabiki wa mchezo huo, ukarabati kabambe wa miundomsingi ya michezo na ufadhili thabiti wa serikali umeiwezesha Nairobi kushinda zabuni ya kuandaa Riadha za Dunia za mwaka 2029.
Tunu hiyo pia imetokana na mafunzo muhimu yaliyopatikana baada ya Nairobi kushindwa katika zabuni ya kuandaa Riadha za Dunia za 2025, ambazo zilipewa Tokyo, Japan.
Nairobi ilirekebisha kasoro zilizojitokeza katika uwaniaji huo na kuboresha mipango yake ili kulishawishi Baraza la Riadha Duniani mara hii.
Rais wa Riadha Duniani, Sebastian Coe, alisema Nairobi iliweka rekodi nzuri zaidi baada ya kurejea na pendekezo imara la kuandaa mashindano ya 2029, ikitumia tajriba ya karibu muongo mmoja ya kuandaa mashindano makubwa ya kimataifa ya riadha.
Coe alisema Nairobi ilianza kujijengea sifa kwa kuandaa Riadha za Dunia za Wasiozidi miaka 18 (Under-18) mnamo 2017, Under-20 mwaka 2021 na Kip Keino Classic, mashindano ya World Athletics Continental Tour Gold yaliyoanzishwa mwaka wa 2020.
“Riadha za Under-18 ya 2017 zilidhihirisha hamu kubwa ya Wakenya katika riadha, huku umati mkubwa ukijaza uwanja wa Kasarani katika kipindi chote cha mashindano.
“Tangu wakati huo, Nairobi imeifanya Kip Keino Classic kuwa mojawapo ya mashindano makubwa ya siku moja barani Afrika, huku mashindano hayo yakiwa sehemu ya World Athletics Continental Tour Gold,” alisema Coe.
Aliongeza kuwa tajriba hiyo iliweka msingi imara wa zabuni ya 2029 iliyojumuisha mipango madhubuti ya uendeshaji pamoja na dhamana za kifedha.
Uwanja wa Kasarani, ambao unafanyiwa ukarabati mkubwa kabla ya kuandaa Kombe la Afrika (AFCON) 2027, miaka miwili kabla ya Riadha za Dunia, ni sehemu muhimu ya maono ya kuandaa Riadha za Dunia kwa mara ya kwanza barani Afrika.
Kiongozi huyo wa riadha duniani alisema Nairobi imeonyesha wazi kuwa wakati umefika wa kuharakisha maendeleo ya riadha nchini Kenya na barani Afrika, huku ikiweka urithi utakaolihamasisha bara hilo na dunia nzima.
Nguvu ya uhusiano wa Kenya na riadha pia imeonekana katika utafiti wa World Athletics kuhusu mashabiki, ambao umeonyesha kiwango cha kipekee cha ushiriki wao.
Asilimia 68 ya Wakenya waliohojiwa walisema wana hamu kubwa ya kufuatilia riadha, ikilinganishwa na wastani wa kimataifa wa asilimia 39. Hii inaifanya Kenya kuwa soko lenye hamu kubwa zaidi ya riadha miongoni mwa masoko yaliyofanyiwa utafiti.
“Kenya ina alama ya juu zaidi ya net promoter score kuliko soko lolote, na riadha ndiyo mchezo wa pili unaofuatiliwa zaidi nchini, baada ya soka pekee,” alisema Coe.
Aliongeza kuwa Kenya ni nchi ya nne duniani kwa idadi ya wafuasi wa kurasa za Riadha Duniani katika mitandao ya kijamii.
Kenya ni nchi ya pili yenye mafanikio makubwa zaidi katika historia ya Mashindano ya Dunia ya Riadha, ikiwa nyuma ya Marekani katika orodha ya medali.
Kenya imeshinda jumla ya medali 182 — dhahabu 72, fedha 60 na shaba 50 — tangu kuanzishwa kwa mashindano hayo mjini Helsinki, Finland, mwaka 1983. Marekani ina medali 649, zikiwemo dhahabu 211, fedha 139 na shaba 119.
Katika Mashindano ya Dunia ya Riadha yaliyofanyika Tokyo mwaka uliopita, Kenya ilishinda medali saba za dhahabu na 11 kwa jumla.
Wanariadha wa Kenya walinyakua mataji yote ya wanawake katika mbio za masafa ya kati hadi marefu uwanjani na mbio za marathoni.
Coe alisema Nairobi iliwasilisha zabuni iliyokuwa na ushindani mkubwa na iliyogusa hisia, akieleza jiji hilo kuwa kitovu kinachokua kwa kasi, chenye nguvu na cha kisasa katika huduma, uchumi, utamaduni na siasa za Afrika Mashariki.
“Kupeleka Mashindano ya Dunia ya Riadha barani Afrika kwa mara ya kwanza kutakuwa jambo la kihistoria. Ilikuwa muhimu mashindano hayo yaje Afrika wakati tunapokuwa na mwenyeji anayefaa, zabuni inayofaa na mazingira yanayofaa. Nairobi imeonyesha wazi kuwa wakati wake umefika,” alisema Coe.
Alisema riadha imejikita katika maisha ya Wakenya na imekuwa chimbuko la wanariadha waliounda historia ya mchezo huo duniani, wakiwemo mabingwa wa dunia Faith Kipyegon, Vivian Cheruiyot, Eliud Kipchoge, Hellen Obiri na David Rudisha.
Wengine ni bingwa wa Olimpiki mara mbili Kip Keino, bingwa mara kadhaa wa dunia wa mbio za nyika Paul Tergat na bingwa mara kadhaa wa dunia wa nusu marathoni Tegla Loroupe.