Michezo

Buyu awinda kuweka historia katika pambano la ubingwa la UBO dhidi ya Ramadhani

Na TOTO AREGE July 23rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

BONDIA wa Kenya, Javan Buyu atamenyana na Mtanzania Idd Ramadhani kuwania taji la Shirika la Universal Boxing Organization (UBO) la Inter-Continental uzani wa lightweigt, katika mashindano ya ndondi yatakayofanyika Jumamosi hii kwenye ukumbi wa Edge Convention Centre jijini Nairobi.

Pambano hilo ni mojawapo ya mapambano 11 yaliyoandaliwa na promota Maurice Odera kupitia UFS BXNG (Ultra Fight Series Boxing), waandalizi wakuu wa ndondi za kulipwa nchini Kenya, kwa udhamini wa SportPesa.

Buyu, ambaye ni bingwa wa Kenya na Afrika Mashariki, ana nafasi ya kutwaa taji lake la tatu la kulipwa na kuwa miongoni mwa mabondia wachache wa Kenya kushinda mkanda wa ngazi ya mabara.

Bondia huyo amesema yuko tayari kwa mtihani huo baada ya kufanya maandalizi ya miezi mitatu bila kuacha jambo lolote kwa bahati.

“Nimekuwa nikifanya mazoezi na kumuomba Mungu kwa ajili ya taji hili. Mimi na timu yangu tumefanya kazi kubwa kujiandaa kwa Julai 25 na tuko tayari. Tumeimarisha kila eneo muhimu litakalotupa ushindi,” alisema Buyu.

Bingwa huyo wa Kenya na wa Pugilist Syndicate of Tanzania (PST) amesema ameboresha uwezo wake wa kutembea ulingoni, kupiga mashambulizi ya kushtukiza na ngumi za mwilini ili kumzidi ujanja mpinzani wake.

“Taji hili lina maana kubwa kwangu kwa sababu litawapa motisha vijana wanaoanza mchezo wa ndondi na pia litafungua milango ya kupigana kwenye majukwaa makubwa duniani,” alisema.

Buyu alitwaa ubingwa wa Kenya Oktoba mwaka jana baada ya kumshinda Christopher Osicho kabla ya kuongeza mkanda wa PST kwa kumcharaza Mtanzania Nasoro Madimba kwa Technical Knockout katika raundi ya tatu mapema mwaka huu.

Amesema tayari amemchunguza Ramadhani kupitia video zake.

“Ni bondia mzuri, ningempa alama saba kati ya 10, lakini nina kila kitu kinachohitajika kumlazimisha akate tamaa. Namwahidi pambano zuri, lakini aandae moyo wa kukubali kushindwa,” alisema.

Hata hivyo, Buyu alikataa kutabiri jinsi pambano hilo litakavyomalizika.

“Mashabiki waje wajionee jinsi nitakavyoshinda,” alisema.

Aidha, aliipongeza SportPesa pamoja na UFS BXNG kwa kuendeleza ndondi za kulipwa nchini kwa kuwapa mabondia nafasi ya kupigania mataji makubwa.

“Naishukuru SportPesa kwa nafasi hii. Wanasaidia kukuza ndondi nchini Kenya na kuwapa wanamichezo nafasi ya kujionyesha. Najivunia kuiwakilisha Kenya na SportPesa,” alisema Buyu, ambaye amesema pia anapigania kutimiza ndoto ya marehemu babake aliyewahi kushiriki ndondi za mashuleni katika Shule ya Upili ya Maranda.

Pia alimpongeza promota Maurice Odera kwa mchango wake katika kukuza mchezo huo.

Kwa upande wake, Ramadhani amesema amewasili nchini kwa lengo moja tu, kutwaa mkanda huo na kurejea nao Tanzania.

“Nataka Buyu ajitayarishe kwa sababu Ramadhani Idd si bondia wa mchezo,” alisema.

Mtanzania huyo, aliyeshinda mapambano tisa kati ya 10 ya kulipwa, anaamini Buyu hajawahi kukutana na bondia wa kiwango chake.

“Buyu alipata shida dhidi ya Martin Shekevuli, lakini mimi nilimwangusha kwa knockout. Hiyo inaonyesha tofauti yetu,” alisema.

Ramadhani alisema kipigo chake pekee kilitokana na uamuzi wa pointi dhidi ya Mrusi Levan Kasaia nchini Poland, uzoefu ambao amesema umemjengea uwezo wa kukabiliana na pambano hilo.

“Nimekuwa kambini kwa karibu miezi mitatu na kila kitu kiko sawa. Nimetumwa kuleta mkanda nyumbani na naamini nitarudi nao Tanzania,” alisema.

Pia aliwataka waamuzi kuhakikisha haki inatendeka.

“Buyu akishinda apewe mkanda. Mimi nikishinda nipewe mkanda. Hicho ndicho ninachoomba,” alisema.