Hofu Cameroon Rais Biya akikosa kuonekana hadharani kwa siku 45
Biya amekuwa nje ya nchi kwa siku 45 na uvumi umetanda kotekote kuhusu hali yake ya afya. Biya, anashikilia rekodi ya kuwa kiongozi wa taifa mwenye umri mkubwa zaidi duniani.
Rais huyo aliondoka Cameroon Juni 7 kwa kile kilichoelezwa na Ikulu kuwa ziara fupi ya kibinafsi barani Ulaya.
Tangu wakati huo hajarejea nyumbani, huku serikali ikikosa kutoa taarifa kuhusu tarehe anayotarajiwa kurejea.
Katibu Mkuu wa Kamati Kuu ya CPDM, Jean Nkuete, aliyeitisha mkutano huo, hakufichua ajenda yake. Katika taarifa, alisema tu kuwa kitakuwa “kikao muhimu cha kazi”.
Haikubainika mara moja iwapo mkutano huo unahusiana na kutokuwepo kwa Biya kwa muda mrefu.
Biya amekuwa madarakani tangu 1982 na kwa miaka mingi amekuwa akiishi Uswizi na mataifa mengine ya Ulaya.
Hata hivyo, kutokana na umri wake mkubwa, safari zake zimeendelea kuzua maswali kuhusu afya yake, mahali aliko na uwezo wake wa kuendelea kuongoza taifa hilo.
Safari ya sasa ndiyo ya muda mrefu zaidi ambayo amewahi kufanya akiwa nje ya nchi.
Baada ya kutoweka kwa muda mnamo 2024, serikali ilipiga marufuku mijadala kuhusu afya ya rais huyo.
Hata hivyo, hatua hiyo haijawazuia viongozi wa upinzani kuhoji hali hiyo.
Mnamo Julai 18, chama cha upinzani cha Cameroon Democratic Union kilitaka mamlaka “kuwapa wananchi maelezo ya kutosha kuhusu uongozi wa taifa”.
Mbunge wa upinzani Jean Michel Nintcheu naye aliandika katika ukurasa wake wa Facebook Julai 17 akitaka Mahakama ya Kikatiba kutangaza kuwa nafasi ya urais i wazi.
Serikali imekuwa ikikanusha ripoti kwamba Biya anapatiwa matibabu nje ya nchi, ikisisitiza kuwa ana uwezo wa kuendelea kuongoza Cameroon akiwa ughaibuni.
Mnamo Aprili, wabunge waliidhinisha kurejeshwa kwa wadhifa wa makamu wa rais ambaye angekuwa wa kwanza kumrithi Biya iwapo nafasi ya urais ingebaki wazi. Hata hivyo, nafasi hiyo bado haijajazwa.
Licha ya kushinda uchaguzi wa urais uliofanyika Oktoba mwaka jana, Biya bado hajateua baraza jipya la mawaziri akifanya kazi na wale waliokuwepo.