Siasa

Salasya sasa adai Sifuna hana umaarufu kisiasa

Na BENSON MATHEKA July 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

HUKU viongozi vijana wakichangamkia kuimarika kwa umaarufu wa Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna, Mbunge wa Mumias Mashariki, Peter Salasya amepuuzilia mbali matokeo ya kura ya maoni uliofanywa na kampuni ya TIFA ambao kinara huyo wa Linda Mwananchi aling’aa.

Akizungumza kupitia kurasa zake za mitandao ya kijamii Julai 24, 2026, mbunge huyo alidai kuwa utafiti huo ulifadhiliwa na Shirika la Kitaifa la Ujasusi (NIS) kwa lengo la kuzua mgawanyiko ndani ya muungano wa upinzani.

Salasya alidai kuwa madhumuni ya utafiti huo yalikuwa kuonyesha kuwa vuguvugu la Linda Mwananchi linaungwa mkono zaidi kuliko muungano wa upinzani, jambo alilosema lilinuia kudhoofisha ushawishi wa viongozi wa upinzani kama kvile Kalonzo Musyoka na Rigathi Gachagua.

Pia aliubeza utafiti huo kwa kejeli, akisema iwapo mwelekeo huo utaendelea, basi Sifuna atakuwa na asilimia 80 ya umaarufu katika utafiti ujao.

Alisisitiza kuwa matokeo hayo hayana uhalali.

“NIS wanafanya kazi ya punda kugawanya upinzani kwa kuonyesha Linda Mwananchi inaungwa mkono zaidi kuliko Muungano wa Upinzani. Tiketi ya Sifuna/Matiang’i sasa ndiyo inaongoza, na hivyo kumfanya Kalonzo na Rigathi waonekane si lolote kisiasa. Kwa kweli, wiki ijayo Sifuna atakuwa na asilimia 80 katika kura za maoni kama mgombeaji bora wa urais,” alisema Salasya.

Kauli za Salasya zilijiri muda mfupi baada ya TIFA kutoa matokeo ya utafiti wake wa hivi punde kuhusu wanaopendelewa kuwania urais, uliomweka Rais William Ruto kileleni kwa asilimia 24 ya uungwaji mkono.

Kwa mujibu wa utafiti huo, Sifuna alishika nafasi ya pili kitaifa kwa kupata asilimia 15, na hivyo kuwa mwanasiasa wa upinzani aliyeongoza kwa umaarufu. Aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani Fred Matiang’i alifuatia kwa asilimia 14, huku kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka akishika nafasi ya nne kwa asilimia 13.