Wataalam watetea kiwanda cha mafuta cha Dangote Lamu
WATAALAMU wa miundomsingi, viwanda na maendeleo ya kimaeneo wameutetea mradi wa Sh2.2 trillioni wa ujenzi wa kiwanda cha kusafisha mafuta ghafi Lamu.
Kiwanda hicho kitafadhiliwa na kampuni ya Dangote Group kutoka nchini Nigeria inayomilikiwa na tajiri wa Afrika, Bw Aliko Dangote.
Licha ya kiwanda hicho kutajwa kuwa na manufaa tele endapo kitawekezwa Lamu, Kenya, wenyeji wanasema kwamba lazima watambuliwe, kushirikishwa na matakwa yao kuzingatiwa kwanza kabla ya hatua zozote za kutekeleza mradi huo kuendelezwa maeneo yao.
Katika mahojiano na Taifa Jumapili, wataalamu, ikiwemo wafanyakazi wa idara za serikali, waliutaja mradi huo wa kiwanda cha mafuta kuwa suluhu ya pekee itakayobadilisha eneo la Lamu kwa uzuri.
Kamishna wa Petroli kwenye Wizara ya Kawi na Petroli nchini, Bw Joseph Otieno, alisema mradi huo utabadilisha eneo hilo kuwa jungu la kiviwanda na maendeleo.
Bw Otieno alisema Kenya imekuwa ikinunua na kusafirisha bidhaa za petroli kwa bei ghali kutoka nje, hasa mataifa ya Mashariki ya Kati kupitia bandari ya Mombasa.
“Watu wa Lamu waondoe shaka. Mradi utatekelezwa kwa kuwazingatia. Kutakuwa na mikutano na makongamano ya kuwaelimisha wenyeji na umma kwa jumla ili wauelewe vyema mradi. Kutakuwa na vikao vya wadau wa serikali, mwekezaji na wakazi wa mashinani Lamu ambao ndio wenyeji wa mradi,” akasema Bw Otieno.
Aliongeza, “Lamu itapanuka kimaendeleo. Barabara zitaboreshwa, biashara zitanoga na sekta zote kunufaika. Hata utendakazi wa bandari ya Lamu pia utaboreka na kufanyika kwa njia ya haraka endapo kutakuwepo na kiwanda cha mafuta.”
Afisa Mtendaji na Mkurugenzi Mkuu wa Zamani wa Mradi wa Bandari ya Lamu, Uchukuzi na Miundomsingi ya Kenya, Sudan Kusini na Ethiopia (LAPSSET), Dkt Silvester Kasuku alisema kuwekezwa kwa kiwanda cha Sh2.2 trilioni cha kusafisha mafuta kutaleta mwamko na taswira mpya ya Lamu kama eneo ambalo kihistoria lilikuwa limetelekezwa.
Dkt Kasuku aliwahakikishia wakazi kwamba serikali itafanya kazi na kushirikiana nao kwa karibu wakati wa kutekelezwa kwa mradi huo.
“Tushafanya kazi kwa karibu na jamii ya Lamu wakati tukitekeleza mradi wa Bandari ya Lamu na tukafaulu. Wananchi wa Lamu watambue kuwa tunawazingatia. Masuala ya ajira, utunzi wa mazingira, ufadhili wa kimasomo na mambo mengine, yote tutayajadili kwa pamoja na kuyakidhi katika kila hatua tutakazopiga wakati mradi utakapokuwa ukitekelezwa eneo hilo,” akasema Dkt Kasuku.
Mwenyekiti wa Zamani wa Muungano wa Save Lamu, Bw Mohamed Athman alitisha kuwa endapo vilio vyao kama jamii kuuhusu mradi vitakaidiwa basi hawatakuwa na budi ila kuelekea mahakamani kuuzuia mradi usifanyike eneo lao.
Afisa Mtendaji wa Muungano wa Wanawake wa Lamu, Bi Raya Famau alishikilia haja ya jamii kuhusishwa kwenye vikao mbalimbali vya umma kutoa maoni kuhuuhusu mradi.
Alisema wao hawapingi mradi ila furaha yao ni kuona haki zao za kijamii zikiheshimiwa.
Naye Mwenyekiti wa Baraza la Wazee wa Lamu, Bw Shee Mbwana alimuomba mwekezaji, Bw Dangote kuweka kikao cha moja kwa moja na wanajamii ili waweze kutoa maoni na vilio vyao kuuhusu mradi.
“Hatuna imani na serikali. Imekuwa ikitudhulumu ardhi zetu kila kunapowekezwa miradi mikuu eneo letu. Sasa tunamsihi Dangote afanye kikao cha moja kwa moja na sisi wanajamii ili tumpe vilio na mapendekezo yetu kabla mradi uendelee,” akasema Bw Mbwana.
Utakapokamilika, mradi huo utakuwa na uwezo wa kusafisha mapipa 700,000 ya mafuta ghafi kwa siku.
Kiwanda hicho ambacho ni kikubwa zaidi Afrika Mashariki kinatarajiwa kujengwa kwa muda wa miaka mitatu.
Kitasambaza bidhaa za petroli iliyosafishwa Kenya na pia nchi jirani, hivyo kupunguza hali ya ukanda wa Afrika Mashariki kutegemea mafuta yanayonunuliwa kutoka nje.
Kiwanda hicho kinalengwa kujengwa eneo la Magogoni karibu na mradi wa Bandari ya Lamu ulioko Kililana, Lamu Magharibi.