Habari

KCPE, KCSE zafufua kumbukumbu za shule kwa Wakenya wanaoishi Uingereza

Na JACKSON NGARI July 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KWA Wakenya wengi, kumbukumbu za mitihani ya KCPE na KCSE huibua picha za usiku wa kukesha wakisoma, wasimamizi wakali wa mitihani na shinikizo kubwa la kufaulu.

Lakini sasa, kile kilichokuwa chanzo cha hofu kimegeuzwa kuwa burudani inayowaleta pamoja Wakenya nchini na ughaibuni.

Nchini Uingereza, jamii ya Wakenya imeanzisha usiku maalum wa maswali na majibu unaotumia maswali ya KCPE na KCSE kama njia ya kuburudika, kukumbushana maisha ya shule na kuimarisha urafiki.

Miongoni mwa walioanzisha shughuli hiyo ni Nicholas Njomo Kamau, mtaalamu wa afya anayefanya kazi katika Huduma ya Kitaifa ya Afya ya Uingereza (NHS).

Alivutiwa na hafla kama hizo zilizoandaliwa Nairobi na jumuiya ya ubunifu ya Qwani.

“Niliona zinafanyika Kenya nikafikiria kwa nini tusizilete hapa, ambako kuna Wakenya wengi. Nimefurahishwa na zilivyopokolewa,” alisema.

Hafla hizo sasa zimefanyika mara tatu katika ukumbi wa Vaha Lounge mjini Northampton. Washiriki huwekwa katika makundi na kujibu maswali ya Hisabati, Kiingereza, Kiswahili, Sayansi na Masomo ya Jamii bila presha ya kufaulu.

Kwa Njomo, uzuri wa wazo hilo ni kwamba karibu kila Mkenya amepitia mfumo wa elimu wa 8-4-4.

“Sote tumewahi kupitia mitihani hiyo,” alisema.

Kilichoanza kama mkutano wa kujiburudisha sasa kimekuwa jukwaa la kujenga urafiki. Washiriki wameunda makundi ya WhatsApp na huendelea kuwasiliana hata baada ya hafla kuisha.

Ingawa washindi hupata zawadi kama vile chupa za pombe, wengi husema zawadi kubwa ni kurejea kumbukumbu za utotoni, walimu waliowapenda, ushindani wa shule na maswali magumu yaliyowasumbua.

Njomo alisema jambo lililomshangaza zaidi ni kuona hata Wakenya wa umri mkubwa wakijiunga na kufurahia hafla hizo.

“Pia tumewaona watu wasiokuwa Wakenya wakija kudadisi. Huondoka wakifurahia muziki, ushindani na mazingira ya Kikenya,” alisema huku akicheka.

Baada ya maswali na majibu, hafla hubadilika kuwa sherehe ya nyimbo za zamani za Kenya. Wageni hufurahia ugali, nyama choma, pilau na mboga za kienyeji huku nyimbo za Gengetone na nyimbo za zamani zikichezwa.

“Tunawaleta ma-DJ wa Kenya kucheza nyimbo zinazotukumbusha enzi za shule,” alisema.

Mwanafunzi wa uuguzi nchini Uingereza, Lynn Saina, alisema hafla hizo huwasaidia Wakenya kupunguza hamu ya nyumbani.

“Kinachonivutia zaidi ni furaha na vicheko. Chumba kilichojaa wageni hubadilika haraka na kuwa familia moja kubwa,” alisema.

Aliongeza kuwa kati ya vipengele vinavyovutia zaidi ni maswali ya methali za Kiswahili, ambapo washiriki hujaribu kukamilisha methali lakini mara nyingi huishia kubuni methali mpya zinazochekesha kila mtu.

Siku ya kwanza, hafla hiyo ilivutia zaidi ya watu 150 uliwathibitishia kuwa Wakenya walikuwa na hamu kubwa ya kumbukumbu zao za shule.