Ker Odungi Randa atetea uamuzi wa Baraza la Waluo kuimba ‘Tutam’
BARAZA la Wazee la Waluo limetetea uamuzi wake wa kushiriki masuala ya kisiasa, likisema hali ya sasa inalazimu wazee kutoa mwongozo kwa jamii badala ya kusalia kimya.
Akizungumza katika Ukumbi wa Ofafa jijini Kisumu, Mwenyekiti wa Baraza hilo, Ker Odungi Randa, alisema wazee walifikia uamuzi huo baada ya mashauriano ya ndani na kubaini kuwa hawawezi tena kunyamaza kuhusu masuala yanayoathiri jamii ya Waluo.
“Sisi kama wazee ni alama ya mwongozo. Tunapoona mambo hayaendi sawa, tuna wajibu wa kutoa mwelekeo,” akasema huku akisisitiza kuwa baraza linaendelea kuunga mkono Serikali Jumuishi ya Rais William Ruto.
Bw Randa pia aliwataka viongozi wa Luo kukoma kushambuliana hadharani akisema migawanyiko ya ndani hupunguza nguvu ya jamii katika majadiliano ya kisiasa na kuwapa nafasi watu wa nje kutumia tofauti hizo kwa manufaa yao.
Kauli yake ndiyo utetezi mkubwa zaidi ambao baraza hilo limewahi kutoa kuhusu kuhusika kwake katika siasa.
Kwa miaka mingi, baraza lilikuwa likisisitiza kuwa jukumu lake ni kuhifadhi utamaduni wa Waluo, lakini msimamo huo umebadilika kufuatia mabadiliko ya kisiasa ndani ya jamii.
Mnamo Julai 2024, baraza liliwahimiza viongozi wa upinzani kufanya mazungumzo yaliyofanikisha kuundwa kwa Serikali Jumuishi.
Baada ya kifo cha aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga mnamo 2025, Ker Randa aliwahimiza Waluo kuendeleza mkondo wa kisiasa ulioanzishwa na marehemu.
Mnamo Mei mwaka huu, baraza lilimuunga mkono hadharani Rais Ruto kuwania muhula wa pili katika mkutano uliofanyika Kisumu na kuhudhuriwa na viongozi wa ODM.
Tamko hilo linakuja wakati ODM inakabiliwa na migawanyiko kufuatia kifo cha Raila. Mrengo unaoongozwa na Seneta wa Siaya Oburu Oginga unaunga mkono ushirikiano na Rais Ruto, huku ule unaoongozwa na Gavana wa Siaya James Orengo ukipinga ushirikiano huo na kudai serikali inaingilia shughuli za chama.
Hapo awali, Orengo amesema Baraza la Wazee wa Waluo haliwezi kuwa mpatanishi huru kwa kuwa tayari limeegemea upande mmoja kisiasa.
Hata hivyo, baraza limekataa madai kwamba limeacha wajibu wake wa kitamaduni, likisema kutoa mwongozo nyakati za sintofahamu ni sehemu ya jukumu lake kama mlezi wa mila na maadili ya Waluo.
Wazee hao pia walidokeza kuwa hivi karibuni watamtangaza mlezi mpya wa baraza hilo baada ya kifo cha Raila Odinga, huku wakithibitisha kuwa tamasha la kitamaduni la Piny Luo litafanyika Kisumu.