Maoni

MAONI: Bila kuwa na ‘mwanajeshi mtiifu’ Kindiki, Ruto atapoteza pakubwa uchaguzini

Na PAUL NABISWA July 29th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MATAMSHI ya Naibu Rais Profesa Kithure Kindiki kuwa hawezi kutoka kwa serikali ni jambo zito sana.

Kwanza ni sauti inayotoka kwa mwanajeshi mtiifu kwa Rais William Ruto. Alikuwa kimbilio na chaguo lake la kwanza baada ya kutimuliwa kwa aliyekuwa naibu wake Rigathi Gachagua.

Gachagua mwenyewe amechafua anga ya Rais Ruto Mlima Kenya sehemu iliyochangia pakubwa ushindi wake katika uchaguzi mkuu wa 2022.

Ila sasa habari zimemfikia kuwa Waziri Wycliffe Oparanya huenda ndiye atakayekuwa mgombea mwenza wa Ruto.

Hesabu hii ya Rais ikiwa itatekelezwa inaweza kumpa majeraha makubwa kuliko angesalia na Kindiki.

Ni wazi kuwa Gachagua amekimbia na idadi kubwa ya wapiga kura.

Swali ni je, Oparanya ataweza kumletea Rais Ruto kura zaidi? Jibu la wazi ni kuwa huenda matokeo yakawa mabaya zaidi kutokana na msisimko wa Seneta Edwin Sifuna.

Oparanya anakabiliwa na upinzani mkubwa kwanza kutoka kwa gavana wake Fernandes Barasa ambaye anadhania kuwa hamtakii mema kwa kuungana na wapinzani wake katika kinyang’anyiro cha ugavana mwaka 2027.

Sasa Rais Ruto atakuwa na kazi ya kuwapatanisha awali ndipo waanze kuzunguka naye nchini. Ilivyo ni kuwa Oparanya hana misuli ya kusukuma kampeni za kitaifa jinsi alivyo Kindiki.

Ikiwa Kindiki na Ruto wataachana basi pacha waliovumiliana katika mateso watakuwa wametengana.

Ikumbukwe Kindiki alikuwa Naibu Spika wa Bunge la Seneti na akaondolewa mamlakani na upande wa Rais Uhuru Kenyatta kwa sababu ya ushirika wake na Ruto.

Wote wamekuwa na misiba tofauti ya kisiasa lakini kilio ni kimoja. Katika kampeni za mwaka 2022 Profesa Kindiki ndiye aliyekuwa wakala mkuu wa Ruto kule Bomas.

Alikubali wadhifa huo licha ya kunyimwa nafasi kuwa mgombea mwenza wa Ruto licha ya wanachama kumdhania kuwa angekuwa chaguo bora.

Hii inatoa sifa ya mtu mvumilivu ila wakati mwingine anajulikana kama ‘fireman”.

Wapo wanaosema kuwa matokeo ya Ol Kalou yamemfanya Rais kumdhania Kindiki kuwa mtu asiyesukuma ajenda ya mlima kwa dhati ya moyo wake.

Jambo lisilo na mjadala ni kuwa ikiwa Ruto atabadilisha mgombea mwenza kutoka kwa Kindiki basi hata asili mia 30 itakuwa vigumu kupata kutoka Mlima Kenya.

DCP itamega sehemu kubwa ya UDA Rais akose uwakilishi wa kitaifa. Kwa waziri Oparanya ngoma hiyo ni kubwa kumzidi.

Ana kibarua kwanza cha kuzima wimbi la Sifuna na gavana Natembeya ambalo limewameza Spika Moses Wetangula na Mkuu wa mawaziri Musalia Mudavadi.

Kwa ufupi ni heri Kindiki kuliko Oparanya.

Paul Nabiswa ni mhariri, NTV