Siasa

Wiper yakanusha Kalonzo alikula ugali na Ruto, yasema madai ni propaganda tupu

Na NDUBI MOTURI July 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

CHAMA cha Wiper Patriotic Front (WPF) kimekanusha vikali madai kuwa kinara wake Kalonzo Musyoka amekuwa na mazungumzo ya kisiasa na Rais William Ruto, kikisema taarifa hizo ni propaganda zinazolenga kuvuruga umoja wa upinzani kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2027.

Naibu Kiongozi wa Wachache katika Seneti ambaye pia ni Seneta wa Kitui, Enock Wambua, alisema madai yanayosambazwa kwenye mitandao ya kijamii na baadhi ya vyombo vya habari kuwa Kalonzo alikutana na Rais Ruto hivi majuzi hayana ukweli wowote.

Alisisitiza kuwa hakujakuwa na mkutano kati ya viongozi hao wawili wala mazungumzo yoyote kuhusu kushirikiana kisiasa kabla ya uchaguzi ujao.

“Ukweli ndio huu, kiongozi wetu hajawahi kukutana na Rais Ruto kwa mazungumzo hayo. Pia hakujakuwa na mazungumzo yoyote kuhusu kushirikiana katika uchaguzi mkuu ujao,” alisema Bw Wambua.

Alitaja taarifa hizo kuwa “habari za uongo, taarifa potovu na propaganda” zilizobuniwa ili kuleta mgawanyiko ndani ya upinzani unaojiandaa kumenyana na serikali ya Kenya Kwanza mwaka 2027.

Bw Wambua alisema wanaosambaza uvumi huo wanajaribu kwa kila njia kudhoofisha kile alichokitaja kuwa serikali mbadala inayoundwa na vyama vya upinzani.

Ili kuondoa utata, seneta huyo alieleza ratiba ya Kalonzo siku ambayo inadaiwa alikutana na Rais Ruto. Alisema alikuwa na Kalonzo siku nzima na kwamba kwanza walihudhuria mkutano na wahariri wakuu wa vyombo vya habari katika hoteli moja jijini Nairobi kabla ya kuelekea mkutano mwingine nyumbani kwa kiongozi huyo.

“Ikiwa Rais Ruto alikutana na mtu anayeitwa Kalonzo siku hiyo, basi hakuwa kiongozi wa Wiper,” alisema.

Wambua alisisitiza kuwa Kalonzo bado ameweka nguvu zake katika juhudi za kuunganisha viongozi wa upinzani ili kuunda muungano mmoja utakaokuwa na mgombea mmoja wa urais dhidi ya Rais Ruto mwaka 2027.

Aliongeza kuwa mkutano mkuu wa wajumbe wa Wiper uliofanyika Oktoba 10, 2025 katika Bustani ya Uhuru ulimuidhinisha Kalonzo kuwa mgombea wa urais wa chama hicho na pia kumpa mamlaka ya kufanya mazungumzo na viongozi wa vyama vingine kwa lengo la kuunda muungano mpana wa upinzani.

Seneta huyo pia alipuuza video inayosambazwa mtandaoni ikidaiwa kuonyesha mkutano kati ya Kalonzo na Rais Ruto. Alisema video hiyo ilirekodiwa Machi 4, 2024 wakati Kalonzo, akiwa mwenyekiti mwenza wa Kamati ya Mdahalo wa Kitaifa (NADCO), alipowasilisha ripoti ya kamati hiyo kwa Rais Ruto pamoja na wajumbe wengine.

Kauli hiyo imejiri wakati uvumi kuhusu miungano mipya ya kisiasa ukiendelea kushamiri, huku Wiper ikisisitiza kuwa mashauriano yanayoendelea yanalenga kuimarisha umoja wa upinzani badala ya kuanzisha ushirikiano na serikali ya Kenya Kwanza.