Kiir atimua Gavana wa Benki Kuu, arejesha aliyemfuta kwa wadhifa huo mwaka jana
JUBA, Sudan Kusini
RAIS wa Sudan Kusini, Salva Kiir Alhamisi alimfuta kazi Gavana wa Benki Kuu Johnny Ohisa, kiongozi huyo akionekana kukumbatia mbinu ya kutekeleza mabadiliko ya mara kwa mara katika serikali yake.
Kiir alitangaza kuondolewa kwa Ohisa kupitia amri iliyosomwa kwenye runinga ya serikali, lakini hakutoa sababu ya uamuzi huo.
Nafasi ya Ohisa imechukuliwa na Addis Ababa Othow, ambaye aliwahi kuhudumu kama gavana wa Benki Kuu kati ya Juni na Novemba mwaka jana.
Rais Kiir amekuwa akitekeleza mabadiliko makubwa katika uongozi wa serikali yake.
Wadadisi wa siasa wanasema hatua hizo zinaashiria juhudi za kuimarisha ushawishi wake huku kukiwa na hali ya kutokuwa na uhakika kuhusu atakayemrithi.
Ohisa, ambaye ni mwanauchumi, amewahi kuhudumu mara kadhaa kama gavana wa Benki Kuu ya Sudan Kusini.
Alirejeshwa katika wadhifa huo mapema mwaka huu baada ya kushikilia nafasi hiyo katika vipindi viwili tofauti hapo awali.
Uchumi wa Sudan Kusini kwa sasa unakabiliwa na changamoto kubwa, zikiwemo kupungua kwa mapato yanayotokana na mafuta, uhaba wa fedha, mfumuko wa bei unaoendelea kupanda na kushuka kwa thamani ya sarafu ya nchi hiyo.