Mbali na nyumba za kupangisha, maghala sasa yavutia wawekezaji
WAKENYA wengi wanapotaka kuwekeza, baadhi hufikiria tu kujenga nyumba za kupangisha au majengo ya kufanyia biashara.
Hata hivyo, kuna aina nyingine ya uwekezaji inayozidi kupata umaarufu kimyakimya ambayo ni uwekezaji katika maghala na majengo ya viwanda ambayo hutumiwa na kampuni kuhifadhi bidhaa na kuendesha shughuli zao za kila siku.
Ni katika mazingira hayo ambapo mfuko wa uwekezaji wa mali isiyohamishika wa ALP REIT umetangaza matokeo yake ya kwanza ya kifedha tangu kuorodheshwa katika Soko la Hisa la Nairobi (NSE) mwezi Machi mwaka huu.
Katika kipindi kilichoishia Juni 30, 2026, mfuko huo ulirekodi faida ya Sh5.8 bilioni, licha ya kutambua mapato ya kodi kwa miezi miwili pekee kutokana na kuchelewa kwa mchakato wa uhamishaji wa mali na upatikanaji wa idhini za kisheria.
Kwa mujibu wa taarifa ya kampuni, ALP REIT ilifunga nusu ya kwanza ya mwaka ikiwa na mali zenye thamani ya dola milioni 45.18.
Kati ya hizo, mali za viwanda na maghala zilithaminiwa kwa dola milioni 26.53 huku dola milioni 14.74 zikisalia kama fedha taslimu kwa uwekezaji wa baadaye.
Mfuko huo, ambao ni wa kwanza nchini kutumia dola za Marekani kama sarafu ya uwekezaji, unasema fedha hizo zitatumika kununua mali ya nne katika mpango wake wa upanuzi.
Majengo yanayomilikiwa na ALP REIT yalikuwa na kiwango cha upangishaji cha asilimia 98, hali inayoonyesha mahitaji makubwa ya maghala ya kisasa yanayotumiwa na kampuni za usafirishaji, biashara na uzalishaji.
Mkurugenzi Mkuu wa ALP REIT Management Limited, Raghav Gandhi, alisema matokeo hayo yanaonyesha msingi imara wa ukuaji wa muda mrefu licha ya mfuko huo kuwa katika hatua za mwanzo.
Hata hivyo, wawekezaji hawatapokea mgao wa muda kwa sasa kwa kuwa kampuni ilikusanya mapato kwa muda mfupi na bado inaendelea na mchakato wa kununua mali nyingine.
Kadri biashara ya mtandaoni, usafirishaji na sekta ya uzalishaji zinavyoendelea kukua nchini, maghala na majengo ya viwanda yanaonekana kuwa sehemu muhimu ya uwekezaji wa siku zijazo.