Iran yanyonga raia wake wawili waliotoa habari za kijasusi kwa Amerika na Israel
TEHRAN, Iran:
NCHI ya Iran imewanyonga raia wake wawili baada ya kupatikana na hatia ya ujasusi na kushirikiana na Israel, vyombo vya habari vya serikali viliripoti hapa Jumatatu.
Haya yanafanyika huku taifa hilo likiongeza utekelezaji wa hukumu za kifo kwa makosa yanayohusishwa na usalama wa Iran.
Walionyongwa ni Omid Behzad na Pouria Safvat, ambao walishtakiwa kwa kuipatia Israel taarifa za kijasusi.
Wawili hao wanadaiwa walituma picha na taarifa za siri wakati wa vita vya mwaka jana na katika mzozo unaoendelea sasa kati ya Amerika-Israel na Iran.
Taarifa hiyo ilichapishwa na chombo cha habari mahakamani, Mizan.
Hukumu hizo zimetekelezwa wakati Iran inaendelea kukabiliwa na hali ya taharuki kutokana na mivutano ya ndani na nje ya nchi.
Mapema mwaka huu, serikali ilikabili maandamano makubwa yaliyotikisa taifa hilo na kuyadhibiti kwa nguvu.
Baadaye, Amerika na Israel zilianzisha mashambulizi mapya dhidi ya Iran mnamo Februari 28, na kuongeza mvutano katika eneo hilo.
Duru ziliarifu kuwa wawili hao walipatia Israel taarifa za kijasusi na kuchangia majeshi yake yalenge vituo vya ukaguzi vilivyokuwa vikilindwa na kikosi cha Iran.
Shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch lilisema Julai 24 kwamba Iran imewaua kwa kunyongwa watu wasiopungua 50 katika kipindi cha miezi minne iliyopita.
Kunyongwa huko kunatokana na madai ya makosa ya usalama wa taifa.
Kundi hilo lilisema baadhi ya waliouawa walikuwa vijana wenye umri wa miaka 18 na 19, huku likikosoa ukosefu wa uwazi katika kesi hizo.
Ujumbe wa kudumu wa Iran jijini Geneva haukujibu ombi la Reuters la kutoa maoni kuhusu taarifa hiyo.
Hata hivyo, Tehran imekuwa ikikanusha mara kwa mara madai ya ukiukaji wa haki za wafungwa.
Wakati huo huo, Rais wa Amerika Donald Trump alisema mazungumzo kati ya nchi yake na Iran yangefanyika Jumatatu.
Hata hivyo, msemaji wa Wizara ya Masuala ya Nje ya Iran, Esmail Baghaei, alisema hakuna mazungumzo yanayoendelea kwa sasa kati ya mataifa hayo mawili.
Vita vya siku 12 vya mwaka jana vilianza katikati ya Juni baada ya Israel kuanzisha mashambulizi ya anga yaliyokuja kuungwa mkono na Amerikan kabla ya kusitishwa baada ya maelewano.
Mzozo wa sasa ulianza mwishoni mwa Februari kufuatia mashambulizi ya Amerika na Israel yaliyohusishwa na shinikizo dhidi ya mpango wa nuklia wa Iran, makombora ya masafa marefu na jinsi serikali ilivyoshughulikia maandamano ya Januari.
Ingawa pande zote zilikubaliana kusitisha mapigano mnamo Juni, mvutano umeendelea, huku juhudi za mazungumzo zikishindwa kufikia makubaliano ya kudumu.