MAONI: Ruto si mwanasiasa mliyezoea pale kijijini, Upinzani wasipotumia akili watapigwa chobo!
KATI ya sasa na mwezi Agosti mwaka ujao, Mkenya hana budi ila kutumia akili sawasawa, na vilevile kumlazimisha mwanasiasa kutumia akili, lau sivyo atemwe kama kikohozi.
Umesalia takriban mwaka mmoja ndipo Uchaguzi Mkuu ufanyike, na huu ndio mwaka ambao wanasiasa huingia mashinani kuwakoroga watu akili kana kwamba wana ukiritimba wa hoja.
Kwa mfano, fununu za ajabu zimeanza kusambaa kote nchini kwamba kiongozi wa chama cha Wiper (WPF) Kalonzo Musyoka, anaelekea kwenye kambi ya serikali, yaani muungano wa Kenya Kwanza (KK) unaoongozwa na Rais William Ruto.
Amekanusha lakini…
Sawa na nguruwe ambaye hujikaanga kwa mafuta yake, Kalonzo akithubutu kufanya hivyo atajimaliza mwenyewe kisiasa na hatawahi kupata nafuu tena wala kutamba katika uga wa siasa za nchi hii.
Serikali ya KK imewaumiza Wakenya mno hivi kwamba mwanasiasa yeyote aliye katika mrengo wa upinzani akithubutu kuingia serikalini atafanya hivyo peke yake, labda na wajinga wachache wanaomzingira kwa kuwa kila soko lina mwendawazimu wake.
Nimesema ni lazima tutumie akili, na tuwashinikize wanasiasa kutumia akili, kwa kuwa enzi ya siasa za tumbo ambapo mwanasiasa kigogo akihongwa na kubadili msimamo wake, na bado kuendelea kuwa maarufu, zimepitwa na wakati.
Nimeandika mara si haba katika kurasa hizi kwamba, hata kigogo wa siasa za janibu za Mlima Kenya, Rigathi Gachagua, akiamua kurejea serikalini iliyomtimua kama paka shume atafanya hivyo peke yake.
Mlima umeasi na kushupaa shingo; haujali wala kubali itakatika ua la.
Sote, wanasiasa na wafuasi wao, tuna lazima ya kutumia akili kwa kuwa mtu tunayejaribu kuondoa mamlakani ana akili tele kichwani.
Rais Ruto si mwanasiasa uliyezoea pale kijijini kwenu na ndio sababu anasema atauvuruga muungano wa upinzani na kuutawanya kwa raha zake.
Hebu angalia, Ruto, mwanasiasa ambaye anapaswa kuwa akitapatapa kwa kuhofia kuzama kisiasa, ameanzisha gumzo la kusisimua na kuuudhi pia – kwamba Kalonzo anaelekea serikalini.
Ruto wa sasa anapaswa kuwa na wasiwasi mwingi kwa kuwa vigogo wa upinzani kutoka kila pembe ya nchi wameungana ili kumwondoa mamlakani, akaibuka na kijana bora nchini, Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna, akaapa kuwa hata useneta ukimtoka, na Ruto ang’olewe mamlakani, ni sawa tu.
Naamini msomaji ungekuwa katika nafasi ya Ruto ungeanza kutetemeka, lakini mwenyewe haonekani kuogopa chochote, amejibadili ngozi kama nyoka, akajifanya maridadi wa kujadiliwa na labda kupiganiwa na wanasiasa wanaotaka kuwa wagombea wenzi wake.
Mara… Ruto anaweza kumtema Naibu Rais Kithure Kindiki wakati wowote; mara… anamtaka Kalonzo; mara… anamtaka Waziri wa Mambo ya Nje Musalia Mudavadi; mara… ODM imempa Gavan awa Homabay Gladys Wanga; mara… Magharibi imempa Waziri wa Ushirika Wycliffe Oparanya; mara… kipenzi chake ni Waziri wa Madini, Uchumi wa Bluu na Masuala ya Bahari Hassan Joho.
Nchi nzima, badala ya kumcheka Ruto kwa kuwa yupo katika nafasi hatari ya kupoteza urais, inazungumzia jinsi alivyo na watu wengi waliotunga foleni kujaribisha bahati ya kuwa manaibu wake.
Ghafla weusi umekuwa weupe! Uvundo umekuwa manukato! Ajabu!
Kwa kubuni mazingira yanayoonyesha kwamba nafasi ya naibu rais inaweza kuwa wazi wakati wowote, Ruto ametukoroga akili nusra tusahau kwamba ana madhaifu yake, wanaisasa walafi nao wakaaza kuimezea mate nafasi ile, wanaotamani kumng’oa wakasahau kufanya kampeni dhidi yake, wakaanza kujiona kama washirika wake.
Kalonzo, aliyeonekana kama mpinzani wake mzito, ambaye alikuwa na nafasi ya kumshinda mwakani, ameshushwa thamani na kuwa mmoja wa hao wanaotaka kuwa watu wa mkono wa Ruto.
Unahitaji akili nyingi ili kuwavuruga na kuwapanga watu hivyo.
Na ndio maana nasisitiza: tusipotumia akili, Ruto atatupanga sote, kufumba na kufumbua tumpate ikulu akihudumu kwa muhula wa pili.
Ikiwa humtaki Ruto, hakikisha unatumia akili zako saa zote ili asikupige chobo.
Douglas Mutua ni mwanahabari Mkenya anayeishi Amerika ([email protected])