MAONI: Mbona Rais Ruto hutukumbusha mara kwa mara kuwa ‘yeye si mwendawazimu’?
KAULI ya Rais William Ruto: I am not a mad man (Mimi si wazimu) inaibua miangwi ya tamthilia za mwandishi wa Nigeria, Ola Rotimi.
Kazi hizo ni: Our Husband Has Gone Mad Again (OUP, 1977), na The Gods Are Not to Blame (OUP, 1971).
Our Husband Has Gone Mad Again (Mume Wetu ni Mwendawazimu) ni kazi ya kitashtiti, inayoangazia maudhui ya ubarakala wa kisiasa, migongano kati ya ukale na usasa, na mafarakano ya ndoa na ya kijinsia.
Kuhusiana na ubarakala wa kisiasa, mhusika mkuu, Major (Mstaafu) Lejoka-Bwown anaona siasa kuwa ulingo wa kujitajirisha, badala ya wenzo wa kuhudumia umma.
Rotimi anawakejeli watawala wa mataifa ya Afrika baada ya uhuru wasiozingatia misingi ya demokrasia.
Mbona Rais Ruto anatukumbusha mara kwa mara kuwa ‘yeye si mwendawazimu’?
Halikadhalika, Rais amesisitiza mara nyingi kuwa ‘yeye si mlevi’ wala ‘mpumbavu’, hasa anapotetea hatua zake za utekelezaji wa sera tata – ambazo aghalabu hupingwa na wananchi.
Baadhi ya sera hizo ni pamoja na mpango wa Bima ya Matibabu (SHA), ujenzi wa nyumba za bei nafuu na mpango wa ufadhili wa wanafunzi wa taasisi za elimu ya juu.
Tathmini inaonesha kwamba, anapolinganishwa na marais waliomtangulia – Mzee Jomo Kenyatta, Daniel arap Moi, Mwai Kibaki na Uhuru Kenyatta, Ruto ndiye rais wa pekee aliyetekeleza kijasiri sera zilizovuruga (disruptive policies) maisha ya Wakenya jinsi tunavyoyafahamu.
Hata pale anapofahamishwa na wataalamu kuhusu athari hasi ya sera hizo, Rais Ruto hupuuzilia mbali ushauri huo – kushadidia kuwa anajua analolifanya.
Je, mbona sasa amekiri, baada ya miaka mitatu – kwamba mfumo wa ufadhili wa elimu ya juu hautekelezeki kamwe?
Aidha, mnamo Juni 25, 2024, kulizuka mageuzi ya vijana (Gen-Z) yaliyochochewa na Mswada wa Fedha wa Mwaka 2024, uliopendekeza nyongeza ya ushuru.
Baada ya vijana wengi kuuawa, Rais Ruto aliamua kutoutia saini mswada huo. Kulikuwa na mantiki gani kuchukua hatua hiyo baada ya maafa kutokea?
Je, huku uchaguzi mkuu wa mwaka 2027 ukikaribia kwa kasi, kuna uwezekano kwamba rais ‘atalegeza misimamo yake mikali’ kuhusiana na mipango, na sera ambazo wananchi wanahisi kwamba zinawakandamiza?
Kuna mafunzo yotote kutokana na mikabala ya utawala wa Rais Ruto? Ndio.
Kwanza, utekelezaji wa sera za kimajaribio zinazodhulumu na kuwakandamiza wananchi ni hatari.
Pili, uongozi wa nchi unapaswa kuwa wa kikoa.
Rais Mwai Kibaki aliwateua wataalamu (technocrats), akawapa uhuru wa kulielekeza dau la uongozi. Kazi yake ikawa unahodha, huku wataalamu wakipiga makasia.
Bitugi Matundura ni mhadhiri ([email protected])