Siasa

Kindiki: Kalonzo hana ajenda, na hawezi kumshinda Ruto 2027

Na CECIL ODONGO August 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

NAIBU Rais Profesa Kithure Kindiki wikendi alimshambulia vikali Kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka, akisema hana ajenda mpya ya kuwaongoza Wakenya baada ya kuhudumu serikalini kwa zaidi ya miaka 40.

Akizungumza katika ziara ya maendeleo Kaunti ya Tharaka Nithi, Profesa Kindiki aliwataka viongozi wa upinzani kuwasilisha sera mbadala badala ya kutegemea siasa za chuki, migawanyiko na ukabila.

“Wale wasioamini maono yetu ya Kenya mpya walete maono yao. Hawawezi kushindana nasi kwa sababu muda wao mwingi wameutumia kuhubiri chuki, migawanyiko na ukabila,” akasema.

Kauli hiyo inajiri huku Bw Musyoka akijitokeza kama mmoja wa vinara wa upinzani wanaolenga kumng’oa Rais William Ruto katika uchaguzi mkuu wa Agosti 2027.

Profesa Kindiki alisema Bw Musyoka ameshindwa kuonyesha mafanikio makubwa licha ya kushikilia nyadhifa mbalimbali serikalini kwa miongo kadhaa.

“Huyo Kalonzo mnayetaka kutuuzia, mlete hapa. Tunamfahamu vizuri kwa sababu alisoma hapa shule ya upili ya Meru. Kama baada ya miaka 40 ya uongozi hajafanya chochote, hana jipya la kutoa sasa,” akasema Profesa Kindiki.

“Aende nyumbani apumzike. Tutamjengea barabara na atuombee kwa sababu huu ni wakati wetu,” akaongeza.

Aidha, Naibu Rais aliwashutumu viongozi wa upinzani kwa kutumia vijana kuzua vurugu badala ya kuwatafutia ajira au kuunga mkono miradi ya serikali ya kuwafaa.

“Kazi ya kiongozi ni kuwasaidia vijana wapate ajira, si kuwalipa Sh200 warushe mawe na kuharibu biashara za wenzao,” akasema.

Profesa Kindiki pia alitoa wito wa amani na umoja, hasa katika eneo la Mlima Kenya, akisema siasa hazipaswi kugawa jamii.

Aliongeza kuwa Kenya Kwanza itatafuta kura kwa kuonyesha rekodi yake ya maendeleo ikiwemo barabara, umeme, maji na miradi mingine badala ya matusi na siasa za migawanyiko.