Habari za Kitaifa

Uhuru aagiza Azimio ifanyiwe mabadiliko, iwatafute Sifuna na Gachagua

Na MOSES NYAMORI August 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MUUNGANO wa Azimio la Umoja One Kenya umeanza mchakato wa kujijenga upya kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027 kwa kuvikaribisha vyama vipya na kuanzisha mazungumzo na makundi ya kisiasa yanayoongozwa na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna.

Katika mkutano wa Baraza la Azimio ulioongozwa kwa njia ya mtandao na Rais mstaafu Uhuru Kenyatta, viongozi hao walikubaliana kuufanyia muungano huo mabadiliko makubwa.

Muungano huo sasa utapewa jina jipya na mawanda yake kutanuliwa ili kuunganisha vyama vyote vya upinzani kabla ya kumteua mgombea mmoja wa urais atakayemenyana na Rais William Ruto.

Katika mabadiliko hayo, vinara Fred Matiang’i wa Jubilee, Peter Munya wa PNU na Seneta wa zamani wa Embu Lenny Kivuti walijumuishwa katika Baraza la Muungano, asasi cha juu zaidi inayofanya maamuzi ndani ya Azimio.

Aidha, vyama vya DP yake aliyekuwa Spika wa Bunge la Kitaifa Justin Muturi, PDP na UMP yake aliyekuwa Gavana wa Meru Kawira Mwangaza vilikubaliwa rasmi kujiunga na Azimio.

Muungano huo pia uliikaribisha tena DAP-K inayoongozwa na Eugene Wamalwa, baada ya chama hicho kusitisha mchakato wa kujiondoa Azimio.

Hata hivyo, Narc-Kenya cha Martha Karua, ambacho sasa kinajulikana kama People’s Liberation Party (PLP), kilijiondoa rasmi mnamo 2024.

Katibu Mkuu wa Azimio Caroli Omondi alisema viongozi wameamua kuanzisha mazungumzo rasmi na chama cha DCP cha Rigathi Gachagua, pamoja na vuguvugu la Linda Mwananchi la Seneta Edwin Sifuna, kwa lengo la kuunda muungano mkubwa zaidi wa upinzani.

Alisema pia Azimio inaendelea kufanya mazungumzo na aliyekuwa Jaji Mkuu David Maraga, ambaye ni Kiongozi wa UGM huku Linda Mwananchi ikitarajiwa kujiunga rasmi mara kitakapokamilisha usajili wake kama chama cha kisiasa.

Kwa mujibu wa Bw Omondi, Linda Mwananchi ndiyo itachukua nafasi ya ODM ndani ya Azimio, kufuatia mgawanyiko ulioikumba chama hicho.

“Tumeamua kupanga upya muungano na kuanza mchakato wa kubadilisha sura na jina la Azimio ili liwe jukwaa linalowakutanisha washirika wote wa upinzani,” akasema Bw Omondi.

Alisisitiza kuwa jukumu la Bw Kenyatta ni kutekeleza wajibu wake kama mwenyekiti wa muungano, akikanusha madai kuwa rais huyo mstaafu ndiye anayepanga mikakati ya kisiasa ya upinzani.

Miongoni mwa sababu za kubadilisha Azimio ni kuhakikisha unaendelea kuwavutia wafuasi wa aliyekuwa Waziri Mkuu marehemu Raila Odinga, huku pia ukivutia vijana wa kizazi cha Gen Z na washirika wapya wa kisiasa.

Inaelezwa kuwa Bw Kenyatta anasukuma ajenda ya upinzani kuwa na mgombea mmoja wa urais ili kuepusha mgawanyiko ulioshuhudiwa mnamo 1992, ambapo wagombea wengi wa upinzani waligawana kura na kumwezesha Rais wa wakati huo Daniel arap Moi kushinda.

Mchanganuzi wa masuala ya kisiasa anayeishi Amerika, Profesa David Monda, alisema mafanikio ya mpango huo yatategemea kujiandaa kwa viongozi wengine wa upinzani kufanya kazi chini ya muungano wa Azimio.

Alisema kufufuliwa kwa Azimio kunaweza kuwa mikakati ya kumweka mbele kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka kama mgombea wa urais, huku ukiwalazimu viongozi wengine wa upinzani kuamua ikiwa wataendelea kushirikiana ndani ya muungano huo au watafuata mkondo tofauti.

Kwa mujibu wa Profesa Monda, upinzani ukiendelea kugawanyika utampa Rais Ruto nafasi kubwa zaidi ya kutetea kiti chake 2027, ilhali muungano mmoja wenye mgombea mmoja unaweza kuongeza ushindani dhidi ya serikali ya Kenya Kwanza.

“Ni wazi Wakenya wanamjua yule mgombeaji ambaye hawatampigia kura lakini bado hawajui watamchagua nani. Hii ndiyo maana lazima upinzani uweke juhudi za kuhakikisha wanaungana,” akasema Profesa Monda.