Siasa

Mwakwere afokea Joho na Nassir kwa kumvumisha Achani kwa muhula wa pili Kwale

Na WINNIE ATIENO August 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MSEMAJI wa jamii ya Wadigo, Bw Chirau Mwakwere, amewashutumu Waziri wa Madini na Uchumi wa Maji, Bw Hassan Joho na Gavana wa Mombasa Abdulswamad Nassir, kwa kumpigia debe Gavana wa Kwale, Bi Fatuma Achani, kuwania muhula wa pili.

Wiki chache zilizopita, Bw Joho alimuunga mkono Bi Achani hadharani na kumtangaza kuwa mgombea anayefaa kuendelea kuongoza kaunti ya Kwale baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.

Hata hivyo, Bw Mwakwere alisema si jambo linalokubalika kwa viongozi kutoka Mombasa kuingilia siasa za Kwale ilhali ODM ina mgombea wake wa kiti hicho.

Aliyekuwa Katibu wa Kilimo Prof Hamadi Boga anawania kiti cha ugavana wa Kwale kupitia chama cha ODM.

“Itawezekanaje viongozi kutoka Mombasa waje hapa Kwale na kumshika mkono mwanasiasa ambaye si mwanachama wa chama chao? Najua hao ni viongozi wa ODM, lakini wanakuja hapa kwetu kumpigia debe mtu ambaye si wa ODM. Hawa ni watu hatari,” alisema Bw Mwakwere.

Aliwataka wakazi wa Kwale kupinga hatua hiyo, akidai kuwa ni dharau kwa viongozi wa ODM katika kaunti hiyo waliodumu ndani ya chama kwa miaka mingi.

“Atakayewaunga mkono hao ni adui wa wamijikenda. Hii ni ishara ya dharau. Profesa Boga amekuwa mwanachama mwaminifu wa ODM na amejitolea kwa chama kwa muda mrefu, lakini sasa anaonekana kuchanganyikiwa hajui afanye nini. Msihofu, tokeni ODM. Msijivunie kusema nyinyi ni ODM damu,” aliwaambia wakazi wa Kwale.