Habari za Kitaifa

Mali ya kifahari ya Wa Iria kupigwa mnada kwa kushindwa kulipa mkopo

Na DOMINIC OMONDI August 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MALI inayohusishwa na aliyekuwa Gavana wa Murang’a, Mwangi wa Iria, inatarajiwa kuuzwa kwa mnada baadaye mwezi huu baada ya kudaiwa kushindwa kulipa mkopo ambao kiasi chake hakijafichuliwa, hali inayoongeza matatizo yake ya kisheria huku pia akikabiliwa na kesi ya ufisadi ya zaidi ya Sh542.6 milioni.

Tangazo la kampuni ya Dalali Traders Auctioneers linaonyesha kuwa nyumba yake ya kifahari iliyoko Karen, Nairobi, pamoja na Edinburgh Mountain Hospital iliyoko Murang’a, zitauzwa kwa mnada mnamo Agosti 25.

Hatua hiyo imejiri chini ya miaka miwili tangu Rais William Ruto amteue Bw Wa Iria kuwa mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Kudhibiti Ununuzi wa Umma (PPRA).

Tangazo hilo linaonyesha kuwa hospitali hiyo iko kwenye shamba la ekari 2.96 katika eneo la Milimani, Kiharu, Murang’a, karibu na Chuo Kikuu cha Murang’a na Chuo cha Matibabu cha Edinburgh. Hospitali hiyo inamilikiwa kikamilifu na Bw Wa Iria kupitia kampuni ya Edinburgh Mountain Hospital Limited.

Mali hiyo imestawishwa kwa jengo la hospitali la ghorofa tano pamoja na maeneo ya kupumzikia.

Nyumba inayotarajiwa kuuzwa iko katika eneo la Karen, kwenye ploti ya ekari 0.48 katika Muiri Lane. Mali hiyo ilisajiliwa kwa jina la Bw Wa Iria na ilitumika kama dhamana ya mkopo uliochukuliwa na Edinburgh College Ltd pamoja na Edinburgh Mountain Hospital Ltd.

Nyumba hiyo ya ghorofa tatu ilikuwa karibu kukamilika na pia ina nyumba ya wageni, maegesho ya magari, pamoja na mipango ya kujenga bwawa la kuogelea, gazebo na nyumba za wafanyakazi.

Bw Wa Iria na kampuni ya madalali hawakufichua jina la mkopeshaji wala kiwango cha mkopo unaodaiwa.

Mbali na madai ya mkopo, Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) pia imewasilisha kesi ikitaka kurejesha Sh542.6 milioni, ikidai fedha hizo zilipatikana kupitia ufisadi na ukiukaji wa taratibu za ununuzi alipokuwa gavana wa Murang’a. Hata hivyo, Bw Wa Iria amekanusha madai hayo na kesi bado iko mahakamani.

Bw Wa Iria ni miongoni mwa viongozi wa zamani ambao mali yao iko hatarini kupigwa minada au kurejeshwa kwa serikali.

Wengine ni aliyekuwa Gavana wa Kiambu Ferdinand Waititu, aliyekuwa Gavana wa Migori Okoth Obado, na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Jubilee Raphael Tuju, ambaye pia amepoteza baadhi ya mali zake kutokana na migogoro ya mikopo.